2014-03-22 11:46:17

Wanawake waandamana Msumbiji kupinga ndoa na watesi wao!


Hivi karibuni, maelfu ya wanawake na wasichana nchini Msumbiji wamefanya maandamano makubwa mjini Maputo kupinga muswada wa sheria unaowataka wanawake waliobakwa na kunyanyaswa na wanaume kuolewa nao kwa walau kipindi cha miaka minne badala ya kufungwa gerezani.

Wanawake na pamoja na wanaharakati wanasema, muswada huu wa sheria una mapungufu makubwa kwani unakwenda kinyume cha haki msingi za binadamu na kwamba, unapaswa kufanyiwa marekebisho makubwa, ili watuhumiwa wanaoendekeza vitendo vya kuwanyanyasa wanawake na wasichana wanapopatikana na hatia, sheria ishike mkondo wake, kama fundisho kwa wote wanaoendekeza mila na tamaduni zilizopitwa na wakati.

Kimsingi muswada wa sheria hii unapata chimbuko lake katika sheria za Msumbiji za Mwaka 1886 zilizoachwa na Wareno wakati wanatawala Msumbiji. Kadiri ya mila na tamaduni za Msumbiji, ndoa za namna hii bado zinakubalika, lakini wanawake na wanaharaki wanasema, umefika wakati kwa Msumbiji kufanya mabadiliko makubwa ili kutetea utu na heshima ya wanawake wa Msumbiji.

Muswada huu wa sheria unataka kuendekeza bado mfumo dume unaowakandamiza na kuwanyanyasa wanawake sehemu mbali mbali za Bara la Afrika.







All the contents on this site are copyrighted ©.