Tume ya haki ya amani ya Baraza la Maaskofu Katoliki Malawi imelaani vikali vitendo
vya uvunjifu wa amani na utulivu vilivyopelekea watu kadhaa kupoteza maisha yao hivi
karibuni nchini Malawi kwenye eneo la Thyolo Goliati. Taarifa kwa vyombo vya habari
inasema kwamba, maisha ya binadamu ni matakatifu na hakuna sababu ya watu kupoteza
maisha kutokana na fujo na vurugu za maandamano ya kisiasa.
Haki ya maisha
na usalama inapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza katika masuala ya kisiasa ili kuepukana
na vitendo ambavyo vinaweza kusababisha watu kupoteza maisha na mali zao. Wananchi
wa Malawi katika ujumla wao wanahimizwa kuwa ni wajenzi wa misingi ya haki, amani
na utulivu na hasa wakati huu wanapojiandaa kwa ajili ya mchakato wa uchaguzi mkuu
nchini humo, unaotarajkiwa kufanyika tarehe 20 Mei, 2014.
Wanasiasa wanatakiwa
kuendesha kampeni zao kwa ustaarabu bila vitisho ili kuweza kupata ridhaa ya wananchi.
Vijana wanahamasishwa kutokubali kutumiwa na wanasiasa kwa ajili ya masilahi yao binafsi
kwa kuwa ni chambo cha vurugu na uvunjifu wa amani na utulivu.