Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya tatu ya Kipindi cha Kwaresima, Mwaka A wa Kanisa
Mpendwa msikilizaji wa Neno la Mungu, tuko tayari Dominika ya III ya Kwaresima kipindi
maalum katika mwaka wa Liturujia kwa ajili ya kujitakatifuza zaidi pamoja na kuyatakatifuza
malimwengu. Neno la Mungu
latualika kutambua zawadi mpya za kimungu. Tunasikia katika somo la kwanza safari
ya Waisraeli toka Misri. Wamekwishavuka Bahari ya Shamu na wanaelekea nchi ya ahadi.
Katika simulizi hilo inaonekana kwamba hapo mwanzoni hali ilikuwa nzuri na waliona
kila kitu kinaongozwa na Mungu, lakini baadaye ilianza kubadilika na hivi mapungufu
ya mahitaji yakaanza kujitokeza, wanakutana na nyoka, joto nk.
Leo tunasikia
shida ya maji, ambayo sasa inajitokeza kwa malalamiko kinyume na Musa. Wanaona Mungu
hawasaidii hata kidogo, amepoteza uaminifu wake na hivi pengine alitaka kuwapeleka
katika kifo badala ya kuwapeleka katika nchi yao!
Mpendwa mwana wa Mungu,
Waisraeli wanajiuliza maswali kadhaa: hivi Mungu yu hai, hivi Mungu yu pamoja nasi
au hapana? Basi tokana na maswali haya yaliyojaa majadiliano, sehemu yalipofanyika
panaitwa Masa na Meriba jangwani wakilishi Kishawishi.
Mpendwa msikilizaji,
shida na malalamiko yanayowagusa wana wa Israeli hayako mbali nasi. Tulipopokea ubatizo
au ndoa au upadre mambo yalikuwa safi, furaha tele na shangwe, lakini polepole tunapokabiliana
na majukumu na haki kuhusu sakramenti hizi huanza kujitokeza magumu na misalaba na
kama hatuko makini malalamiko huanza na hata kinyume na Mungu. Basi kwaresima hii
ni kusali kuomba ili tupate kutunza upole na uvumilivu wa moyo. Mkristu anavumilia
mpaka Kalvari, hakuna kurudi nyuma kamwe.
Mt. Paulo anapowaandikia Warumi na
hivi kutuandikia sisi hivi leo, anakazia tumaini lililojisimika katika mapendo ya
Mungu kwetu pasipo kutegemea udhaifu wetu au wema wetu bali ni mkamilifu siku zote.
Ndiyo kusema upendo wake haute gemei kazi nzuri tunazofanya. Mungu huwapenda hata
adui zake, kinyume nasi ambao mwelekeo wetu ni kuwachukia adui zetu. Basi katika kwaresima
hii tufunge ili tuweze kufungua macho ya mapendo kwa wote kama ambavyo mwanga ni kwa
wote.
Katika Injili tunakutana na picha ya mwanamke msamaria aliyekutana na
Masiha katika kile kinachoitwa kisima cha Yakobo. Katika mantiki ya wakati ule kisimani
palikuwa ni sehemu ya wanakijiji kukutana. Wachungaji walifika pale kwa ajili ya kunywesha
mifugo yao. Wafanyabiashara walikutana na wanunuaji wa mali zao. Si haya tu bali pia
akina mama walikwenda kuteka maji kwa ajili ya familia zao. Injili ya leo inachukua
sehemu mojawapo ya mikutano mbalimbali kama tulivyokwisha itaja. Bwana anakutana na
mwanamke Msamaria aliyekuja kuteka maji.
Yesu alikuwa amechoka kwa safari
na alikuwa anapumzika pale akiwasubiri Mitume waliokuwa wamekwenda mjini kununua chakula.
Kwa vyovyote vile Bwana hakuwa na kichoteo kwa ajili ya kuchukua maji na kunywa na
kwa kuwa kisima kilikuwa kirefu yapata meta 32 hivi asingeweza bila kichoteo. Basi
anaomba msaada toka kwa mama msamaria. Mara moja mama huyu atagundua, nadhani kwa
sauti kuwa huyu ni mgalilaya!
Mpendwa msikilizaji, katika hili, kinachofuata
ni maswali: hivi inawezekanaje mgalilaya akaomba msaada kwa msamaria? Ni kwa uwezo
gani mtu huyu aweza kuvunja mila ambayo hairuhusu mwanamme akiwa peke yake kuongea
na mwanamke asiyemfahamu? Katika hili sheria yao iliruhusu kuongea maneno machache
wakati mtu anahitaji maelekezo fulani! Hata hivyo, Bwana anavunja miiko hii, akitaka
kuondoa utengano uliojikita katika mila na desturi. Anachotafuta ni usafi wa moyo
na si wasiwasi na mashaka ya nje.
Mpendwa msikilizaji, kitendo cha Bwana kukutana
na mwanamke msamaria pale kisimani katika Injili ya Matayo kinatupa tafakari ya ndani
kabisa. Kisima ni sehemu ya makutano ya wachumba ambao baadaye wataoana. Katika Agano
la Kale taifa la Israeli lilitambuliwa kama mchumba wa Mungu. Lakini tukisonga mbele,
tunaona jinsi mchumba Israeli alivyovunja agano na Mungu, na hasa anapomsaliti mchumba
wake wa kwanza na kuanza kwenda kwa wachumba wengine: Wamisri, Waasiria, Wababilonia,
Wapersia na mwishoni Warumi!!
Basi tunaporudi katika Injili ya leo tunakutana
na huyu mama msamaria ambaye yuko pale kuwakilisha taifa la Israeli ambalo halikuwa
aminifu mbele ya Agano na Mungu. Kwa hakika mama huyu alikuwa malaya. Kumbe Bwana
anapokutana naye anataka kumrudisha katika pendo la Mungu, anataka arudi katika uhuru
kamili na ajipatie heshima yake aliyoipoteza katika jumuiya. Je, sisi tuko mbali na
mambo haya? Tutafakari!
Mpendwa msikilizaji, Bwana anataka kumpatia mama huyu
chakula na maji yakatayo kiu daima na wala si maji ya kisima kile cha Yakobo. Maji
ya kisima cha Yakobo ni ishara ya mambo yote mtu ayatafutayo akifikiri yatamaliza
kiu yake na badala yake huiongeza na hata kukata tamaa. Mpendwa jaribu kufikiri unapotenda
dhambi ukifikiri itakupa furaha, baada ya muda unaanza kurudi nyuma na kujiuliza maswali
kadhaa: hivi kwa nini nimefanya jambo hili, Je ningekamatwa?, Basi shida na msongo
wa maswali huendelea mpaka pale tu utakapoondolewa dhambi hiyo na ndipo utatulia.
Mpendwa msikilizaji katika hili kumbuka utulivu na furaha vinapatikana katika kutimiza
mapenzi ya Mungu tu. (Roho yangu haitulii mpaka hapo itakapotulia katika Mungu, Mtakatifu
Agustino wa Hipo).
Mpendwa mwana wa Mungu, Bwana anapendekeza na kutoa maji
mapya yakatayo kiu daima, nayo ni roho ya Mungu, ndiyo usema anayejikabidhi kuongozwa
na roho wa Mungu atapata utulivu na furaha moyoni na maishani mwake. Mama msamaria
anakuwa mfano wa ukuaji wa kiroho, maana mwanzoni alimwona Bwana kama msafiri na kisha
akawa Bwana, polepole Nabii, Masiha na mwishoni ni Mkombozi wa ulimwengu. Nasi wapendwa
kukutana na Mungu kwa njia ya Neno lake au jumuiya Kanisa, kunatupasa kutufanya tukue
kiroho na kuanza maisha mapya. Mwanamke msamaria anaacha mara moja mtungi wa maji
baada ya kutambua Masiha na anakwenda kutangaza habari njema hiyo, habari ya furaha.
Ni wajibu uleule tunaopaswa kuutenda mara tu tunapogundua nani ni Masiha yaani, aliyekuja
kuleta uhuru na kukarabati upendo msingi uliokusudiwa tangu kuumbwa ulimwengu.
Mpendwa
msikilizaji wa Radio Vatican, ninakutakia furaha na matumaini katika maisha yako daima
ukimtanguliza Mungu na kwa namna hiyo kuijua hekima ya kweli itokayo kwa Mungu aliye
kisima kipya cha wokovu. Tumsifu Yesu Kristo.
Tafakari hii imeletwa kwako
na Padre Richard Tiganya C.PP.S.