2014-03-21 09:39:01

Tafadhali sana! Msiige kila kitu!


Mwanasheria mkuu mstaafu wa Kenya, Amos Wako amewawaonya Wabunge wa Bunge Maalum la Katiba linaloendelea nchini Tanzania kuwa makini na wala wasikubali kuiga mambo ya Katiba za nchi nyingine bila kuangalia uhalisia wa maisha na mazingira ya watanzania wenyewe. Wabunge wazingatie kwanza kabisa haki msingi za binadamu, umoja wa kitaifa, ustawi na mafao ya watanzania wengi.

Amos Wako ameyasema hayo wakati alipokuwa anashirikisha mang'amuzi ya mchakato wa utungaji wa Katiba Mpya ya Kenya miaka kadhaa iliyopita. Anasema, mchakato wa Katiba Mpya nchini Tanzania unaendelea vyema na kwamba, unawashirikisha watu kutoka katika makundi mbali mbali na baadaye Watanzania watapata fursa ya kuupigia kura ya maoni, kuukubali muswada au kuukataa. Kumbe, ni vyema wabunge hao wakatumia vyema dhamana waliyokabidhwa na watanzania wenzao ili kuweza kupata Katiba bora zaidi ambayo kimsingi ni Sheria Mama.

Amewaomba Wabunge kuzingatia misingi ya haki, amani na utulivu; kwa kujenga utamaduni wa kusikiliza kwa makini na kupingana kwa nguvu ya hoja, kwa ajili ya mafao na ustawi wa watanzania. Wabunge wasikubali kushindwa na kishawishi kitakachowatumbukiza katika machafuko ya kisiasa kama ilivyojitokeza katika sehemu mbali mbali za dunia wakati wa mchakato wa kuandika Katiba Mpya. Wajitahidi kuhakikisha kwamba, Katiba Mpya inakuwa ni Mali ya Wananchi kwa kuwahusisha wananchi wenyewe. Mchakato wa kupata viongozi watendaji wakuu wa Serikali umebainishwa vyema katika Mchakato wa Katiba, hali inayoonesha umuhimu wa kukuza na kudumisha misingi ya ukweli, uwazi na uwajibikaji.

Imeandaliwa na Rodrick Minja,
Dodoma.







All the contents on this site are copyrighted ©.