2014-03-21 08:24:23

Siku ya Misitu Duniani kwa Mwaka 2014


Mwezi Novemba 2012 Baraza kuu la Umoja wa Mataifa lilianzisha Siku ya Misitu Duniani, inayoadhimishwa kila Mwaka ifikapo tarehe 21 Machi. Lengo ni kuwahamasisha watu kulinda, kutunza na kuendeleza misitu kwa ajili ya kizazi cha sasa na kile kijacho.

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Ban Ki-Moon katika ujumbe wake kwa Siku hii, inaitaka Jumuiya ya Kimataifa kulinda misitu kwani ni kikolezo kikubwa cha maendeleo ya mwanadamu sanjari na mapambano dhidi ya umaskini na ukosefu wa usalama wa chakula duniani. Utunzaji bora wa misitu unaweza kusaidia kudhibiti kwa kiasi kikubwa madhara yanayosababishwa na mabadiliko ya tabianchi.

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa anasema kwamba, zaidi ya watu billioni 1.6 wanategemea misitu kwa ajili ya kupata chakula, nishati, makazi na pato katika maisha. Takwimu za Shirika la Afya Duniani, WHO, zinaonesha kwamba, watu asilimia 65% hadi 80% wanategemea dawa zitokanazo na misitu kama chanzo cha tiba kwa magonjwa yanayowasibu.

Misitu ni kikolezo kikubwa cha maendeleo endelevu katika viwango mbali mbali na inachangia walau asilimi 1% ya Pato Ghafi la Taifa na kwamba, misitu ni mhimili mkubwa katika sekta ya kilimo, viwanda, nishati na matumizi ya nyumbani. Umoja wa Mataifa unawataka wadau mbali mbali kuhakikisha kwamba, wanatumia siku hii kwa ajili ya kuhamasisha watu juu ya utunzaji bora wa misitu kwa ajili ya mafao ya wengi.







All the contents on this site are copyrighted ©.