2014-03-21 07:51:19

Mjadala wa kuruhusu matumizi haramu ya dawa za kulevya ni kwa mafao ya nani?


Bodi ya Kimataifa ya Kudhibiti Dawa za Kulevya iliyopewa dhamana ya kuhakikisha kwamba, itifaki zilizoridhiwa na Jumuiya ya Kimataifa kuhusu udhibiti wa dawa za kulevya unatekelezwa katika ni jambo la msingi sana. RealAudioMP3

Haya yamo katika taarifa yake inayohusu Hali ya Dawa za Kulevya ya Umoja wa Mataifa kwa Mwaka 2013, inaonesha madhara ya matumizi haramu ya dawa za kulevya katika: uchumi na jamii; afya na usalama wa raia; uhalifu na vitendo vya jinai, tija na uzalishaji pamoja na utawala bora.

Bodi hii imeonesha msimamo wake kwa kutokubaliana na maamuzi yanayotolewa na baadhi ya nchi duniani kwa kutaka kuruhusu matumizi ya dawa za kulevya, kama ilivyojitokeza hivi karibuni nchini Uruguay na katika baadhi ya majimbo nchini Marekani. Baadhi ya watu wanaounga mkono mwelekeo huu mpya wanasema kwamba, gharama ya kudhibiti biashara haramu ya dawa za kulevya ni kubwa mno na ina hatari kubwa.

Bodi ya Kimataifa ya Kudhibiti Dawa za Kulevya inasema kwamba, hoja hii haina nguvu kwani Serikali nyingi zinaendelea kupata kodi kubwa kwa kuuza vileo na tumbaku, lakini gharama ya afya inayotokana na matumizi ya vileo na tumbaku ni kubwa mno ikilinganishwa na kodi inayolipwa kwa serikali.

Ikiwa kama Serikali mbali mbali duniani zitaendelea kuruhusu matumizi haramu ya dawa za kulevya. Itabidi pia kuongeza nguvu katika mchakato wa ulinzi na usalama, kwani takwimu za kimataifa zinaonesha kwamba, watu wengi waliofikishwa kwenye mkondo wa sheria ni wale ambao wamekutwa na makosa yanayohusiana na ulevi pamoja na matumizi haramu ya dawa za kulevya.

Baadhi ya hoja zinazotolewa ni kwamba, ikiwa kama matumizi ya dawa za kulevya yataruhusiwa, wafanyabishara waliokuwa wanategemea sana biashara hii kama chanzo cha pato lao watakamwa. Lakini, Bodi ya Kimataifa inasema, hoja hii haina nguvu kwani wafanyabiashara wa dawa haramu za kulevya wanaweza kuingia katika soko halali la dawa za kulevya pamoja na kuendeleza soko haramu la dawa hizi kama ilivyo katika biashara ya sigara duniani. Asilimia 9% hadi 20% ya Soko la Sigara Uingereza inatokana na biashara ya magendo ya sigara na hivyo wanaikosesha Serikali kodi halali wanayopaswa kulipa.

Takwimu za Kimataifa zinaonesha kwamba, kumekuwepo na ongezeko kubwa la ajali barabarani zinazotokana na matumizi haramu ya dawa za kulevya, jambo linaloendelea kuhatarisha maisha ya watu, mali na maiundo mbinu inayojengwa kwa gharama kubwa. Matumizi ya dawa haramu za kulevya ni chanzo kikuu cha vifo miongoni mwa watu wenye umri kati ya miaka 15 hadi 64. Ni chanzo kikuu cha ongezeko la mauaji na vitendo vya jinai. Madhara ya matumizi haram ya dawa za kulevya yanaweza kupunguzwa kwa njia ya elimu makini, kuzuia na kuponya kama mwelekeo sahihi katika kupambana na matumizi haram ya dawa za kulevya.

Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki inasema matumizi haramu ya dawa za kulevya yanauletea mwili na afya ya binadamu hasara kubwa. Matumizi yake ni kosa kubwa, isipokuwa kwa misingi tu ya tiba. Utengenezaji wa holela na usafisrishaji wa dawa za kulevya ni mazoezi mabaya. Yanayounda ushirika wa uovu, kwa kuwahimiza watu kuingia katika mazoea yaliyo kinyume kabisa cha sheria ya maadili. Kumbe, kuruhusu matumizi ya dawa za kulevya ni jambo ambalo ni hatari na wala halina mvuto! (Rejea, KKK no 2291).

Imehaririwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.