2014-03-20 10:52:24

Ulimwengu wa digitali unapaswa kuinjilishwa kwa njia ya imani tendaji!


Monsinyo Paul Tighe, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la Mawasiliano ya Jamii anabainisha kwamba, mabadiliko makubwa ya maendeleo ya sayansi na teknolojia ya mawasiliano ya jamii ni changamoto kwa watu kubadili njia na mfumo wa mawasiliano unaojikita zaidi katika majadiliano. RealAudioMP3

Huu ndio mwelekeo unaotakiwa na vijana wa kizazi kipya wanaoendelea kuogelea katika ulimwengu wa digitali, tofauti na Makleri waliozoea utamaduni wa kuzungumza na kusikilizwa pengine hata bila ya kuulizwa maswali.

Maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari yanawezesha mchakato wa mawasiliano kuwa wa njia mbili: Hili ni jukwaa ambalo watau wanajadiliana, wanashirikishana, wanaweza kuelewana au kusigana. Ni mahali pa kuchangia hoja, hapa watu wanauliza maswali msingi ili kupatiwa majibu muafaka yatakayoweza kukidhi hamu ya mioyo yao! Katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi ya teknolojia ya habari mambo makuu matatu yanajenga msingi wa mawasiliano: Kusikiliza, Kushirikisha na Kutia moyo!

Haya ndiyo mambo makuu ambayo yamelisukuma Kanisa kujikita katika matumizi ya njia mpya za mawasiliano ya kijamii, kama inavyojionesha kwa namna ya pekee kwa Baba Mtakatifu Francisko ambaye anatumia mitandao ya kijamii na kwamba, idadi ya wale wafuasi wake hadi sasa ni zaidi ya million kumi.

Hata katika Injili, Yesu aliweza kuzungumza mambo makubwa kwa kutumia maneno macheche tu! Kwa mfano Kheri za Mlimani ni muhtasari wa Mafundisho makuu ya Yesu kama ilivyo pia kwa Sala ya Baba Yetu wa Mbinguni. Huu ni mwaliko na changamoto kwa Maaskofu pamoja na viongozi wengine wa Kanisa kuangalia jinsi wanavyoweza kutumia maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari kwa ajili ya kutangaza Habari Njema ya Wokovu na Kweli za Kiinjili.

Mitandao ya kijamii ni jukwaa lenye mazuri na mapungufu yake. Hata Baba Mtakatifu Francisko alipoanza kutumia mitanao hii alikumbana na upinzani hata wakati mwinginie na maneno ya kashfa na kejeri, lakini ni mambo ambayo hayakumkatisha tamaa! Kuna baadhi ya watu walitaka kuhakikisha kwamba, anafunga akaunti yake mara moja, lakini kwa bahati mbaya hawakufua dafu!

Baba Mtakatifu Francisko ameendelea kutumia mitandao ya kijamii kadiri ya uwezo wake bila woga wala makunyanzi. Katika mtandao wa Baba Mtakatifu @Pontififex, anatuma ujumbe, lakini si mara zote anawajibu. Makanaisa mahalia wanaweza pia kujenga na kuendeleza jukwaa hili kwa kutumia kanuni ya auni.

Matumizi ya mitandao ya kijamii yanayofanywa na Baba Mtakatifu yanaonesha mafanikio makubwa kwa mfano wakati alipowaalika waamini kujiunga naye kusali kwa ajili ya kuombea amani nchini Syria, kulikuwa na mwitiko mkubwa, licha ya ukweli kwamba, Kanisa pia lilitumia njia za kawaida za mawasiliano ya Jamii ili kufikisha Ujumbe wa Baba Mtakatifu kwa watu wengi zaidi. Katika kipindi cha muda mfupi tu, waamini kutoka katika Majimbo, Parokia za Jumuiya zao walijikusanya na kuanza kuwashirikisha wengine ujumbe kutoka kwa Baba Mtakatifu Francisko.

Monsinyo Paul Tighe anasema, Vatican inaendelea kuboresha mfumo wake wa kupasha habari kwa kusoma alama za nyakati. Leo hii kuna ushirikiano mkubwa kati ya vyombo na taasi za habari za Vatican kama vile: Kituo cha Televisheni cha Vatican, Radio Vatican, Gazeti la L’Osservatore Romano; vyombo vyote hivi vinapatikana kwenye mtandao wa habari ujulikanao kama News.va. Kwa maneno machache maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari yanawawezesha watumiaji kutembea na Baba Mtakatifu mifukoni mwao!

Maendeleo yote haya ni fursa kwa vijana kujieleza, kujifunza, kuhabarishana sanjari na ujenzi wa urafiki. Hadi sasa wataalam wa mawasiliano ya kijamii hawana uhakika wa dira na mwelekeo wa njia hizi za mawasiliano kwa siku za usoni, kwani s itu kwamba zinaleta mabadiliko, bali pia watumiaji wa mitandao hii wanabadilisha namna yao ya kufikiri na kutenda, ikilinganishwa na miaka kadhaa iliyopita. Kuna mabadiliko makubwa ya jinsi ya kujenga na kuimarisha Jumuiya za waamini wanaojisikia kuwa ni sehemu ya Kanisa linalopaswa kushuhudia imani yake.

Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita alishawahi kudokeza kwamba, kuna haja ya kufanya tafakari ya kina na kuangalia taalilimungu inayobebwa kwenye mitandao ya kijamii, ili kuweza kuitumia kikamilifu! Waamini wajifunze lugha ya utamaduni mpya wa digitali, ili kuweza kumwilisha Injili ya Kristo katika jukwaa hili jipya la mawasiliano ya Jamii. Waamini wawe makini kuchagua yale yanayofaa katika maisha na utume wao kama Wakristo na kuangalia mambo ambayo pia yanapaswa kubadilishwa.

Baba Mtakatifu Francisko anasema, Kanisa haliwezi kuwa mtazamaji katika matumizi ya mitandao ya kijamii, bali linapaswa kuingia na kushiriki kikamilifu katika mchakato wa kuitakatifuza mitandao hii kwa njia ya ushuhuda wa imani tendaji. Jukwaa hili linawakusanya mamillioni ya watu wanaotumia muda mrefu kupata na kutoa habari.

Kanisa lisipojiingiza kikamilifu katika Jukwaa la mitandao ya kijamii, litashindwa kuwafikia waamini katika uhalisia wa maisha yao! Hii ni hija ya ambayo inapania kumwezesha mwamini kukutana na kuzungumza na Yesu; kwa kujali na uvumilivu mkubwa; kuwajibika na katika ukweli; kwa kuzama katika tamaduni na lugha za mitandao ya kijamii bila kusahau kubeba ”mtumba wa imani tendaji”.

Meandaliwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.