Watanzania wanamkumbuka Marehemu Padre Egidio Guidi
Ndugu Egidio Guidi alizaliwa katika Parokia ya Premilcuore – Jimbo la Forli, Provinsi
ya Toscana, mnamo tarehe 17 Machi 1933. Akiwa na miaka mitatu alifiwa na mama yake
na kulelewa na Edvige Mussolini, Dada wa aliyekuwa Benito Mussolini, (Fashisti) na
mtawala wa nchi ya Italia wakati wa vita ya pili ya dunia. Angali bado mdogo na akiwa
na miaka 12, alijiunga na seminari ndogo.
Mwaka 1950, baada ya kumaliza masomo
yake ya Sekondari na akiwa na umri wa miaka 17 tu alijiunga na ndugu Wakapuchini katika
Provinsi ya Toscana kwa kuanza malezi ya Novisiati. Mwaka moja baadaye Septemba 8,
1951, alisherekea nadhiri zake za kwanza. Miaka mitatu baadaye Septemba 12, 1954 alifunga
nadhiri zake za daima. Akiwa na miaka 25, Machi 22, 1958 Ndugu Egidio alipewa daraja
la Upadre.
Umisionari: Kutokana na hamu yake ya kuwa Mmisionari katika
nchi za Afrika, aliomba kwa wakubwa wake kuja katika nchi ya Tanganyika (Tanzania)
na ombi lake lilikubaliwa. Tarehe 2, Juni 1963 akiwa na wenzake wanne, akiwa na umri
mdogo kuliko wenzake, walikabidhiwa, msalaba wa Umisionari, na ndipo tarehe 6 Juni,
1963, kwa kutumia meli, walianza, safari ya kuja katika nchi ya Tanganyika (Tanzania).
Baada ya meli yao kutua nanga katika bandari ya Dar es salaam alielekea Pugu, ambapo
kwa muda alikaa katika parokia hiyo.
Mwezi Julai, 1963 pamoja na wenzake walianza
safari kuelekea Dodoma kupitia Iringa ambapo tarehe 28 Julai 1963 walienda sehemu
ya Kondoa kwenye Parokia ya Haubi na Itololo kwa ajili ya kujifunza lugha ya Kiswahili.
Utume
na Sehemu alizoishi kufanya kazi: Mnamo Desemba 8, 1963 alielekea katika Parokia
ya Mpwapwa. Katika utume wake kwenye Parokia ya Mpwapwa kama Paroko msaidizi, Utume
wake ulihusisha kazi za kiofisi, shule za msingi, sekondari na Chuo cha Ualimu. Kwa
usafiri wa lori aliloendesha mwenyewe aliweza kuzunguka eneo kubwa la vigango vya
Kongwa hadi Mlali (wakati huo). Ilichukua muda kwa baadhi ya Wakristu kufahamu kama
ni Padre kwani walifikiri ni dereva tu wa lori mpaka walipomwona tena altareni kwenye
adhimisho la MisaTakatifu.
Akiwa bado katika Parokia ya Mpwapwa aliweza pia
kusimamia ujenzi wa nyumba ya Mapadre, Masista, kiwanda cha kupasua mbao, makanisa
ya Vigango vya Kisokwe, Godegode na Tubugwe, na pia kuanzisha jengo la chekechea.
Changamoto iliyotokana na Uhuru wa Tanganyika (1961) ilikuwa baada ya uhuru baadhi
ya watu hawakuweza kutofautisha Wamisionari na Wakoloni.
Wakati mwingine watu
hawakuweza kuwasaidia au kuwasikiliza wakifikiri ni Wakoloni waliosalia. Baadaye watu
waliendelea kuwazoea na kuwapokea na kuwaona kweli wao ni Wamisionari na sio wakoloni
waliosalia.
Kutokana na hitaji katika Parokia ya Kongwa, mnamo Oktoba 10,1968,
alihamia Kongwa sehemu ya Morisheni, walipokaa Washeli- sheli kutoka Mauritania. Akiwa
Paroko Msaidizi wa Kongwa, mwaka 1971, alitumwa kwenda Kigango cha Mlali ili kujenga
Kanisa, nyumba ya Mapadre, nyumba ya Masista, shule ya chekechea – kusudi Mlali iwe
Parokia baadaye. Ujenzi huo ulikamilika mwaka 1975, kisha Askofu Mathias Isuja alipofika
kubariki Jengo, alitangaza Mlali kuwa Parokia. Ndugu Egidio akabaki Mlali na kuwa
Paroko msaidizi.
Hatimaye Januari 20, 1977 alipata uhamisho kwenda Parokia
ya Mbuga na kuwa Paroko, baada ya kukosekana mtu wa kumtuma Mbuga. Ndugu Egidio alijitolea.
Mbuga ilihudumiwa na Mapadri Wapasionisti tangu mwaka 1940 hadi mwaka 1958 ilipotangazwa
kuwa Parokia. Ndugu Egidio, alikaa kwa miaka 24 na miezi 11 Mbuga akiwa kama Paroko.
Kama paroko hakubaki tu ofisini kuwasuburi waumini, ila alikuwa pia dereva, na fundi
wa mambo mbalimbali, na pia aliweza kutoa huduma za Kiroho na kusimamia ujenzi wa
vigango vipya vya Uleling`ombe, Galigali, Matonya, Mandasi, Mtamba na Kizi.
Kwa
vile hapakuwa na hospitali eneo hilo, alilazimika kuwapeleka wagonjwa umbali wa Kilometa
84 kwenye hospitali ya Mpwapwa kwa nyakati zote hasa usiku, na pale wenyeji walimwita
jina“ Chausiku” kwani wakati mwingine ilibidi kusafiri usiku kumfikisha mgonjwa hospitali,
au kurudi usiku kwenye kituo chake cha Parokia ili Waumini wasije wakakosa huduma
za kiroho. Akiwa katika Parokia hiyo aliweza kuwapeleka vijana wengi kwenye miito
mbalimbali, kwa upande wa mapadre wapo mapadre 13 na kwa upande wa Masista hata yeye
hajui ni wangapi amewapeleka Utawani.
Mnamo Julai 2002 aliteremka tena toka
Parokia ya Mbuga hadi Parokia ya Kongwa ambapo alikuwa Paroko msaidizi hapo. Hapo
ndipo Mhudumu wa Provinsia alipomwomba kuwa karibu na kuratibu masuala ya ujenzi wa
Kanisa la Mkoka. Mei 24, 2005 kwa maridhiano ya Mhashamu Askofu Mathias Isuja – aliyekuwa
Askofu wa Jimbo la Dodoma na kibali kutoka kwa Mhudumu wa Provinsia aliwekwa kuwa
Paroko wa Parokia ya Mkoka.
Lengo lilikuwa kuendeleza na kukamilisha ujenzi
wa nyumba ya Mapadre na Jengo la Kanisa. Hata hivyo Egidio hakuishia hapo, kwani alianzisha
ujenzi wa shule ya awali ya Nazareti, nyumba ya masista, stoo, jiko, mradi wa mashine
ya kukamua alizeti kwa lengo la kusaidia jamii na kutegemeza Parokia.
Toka
wakati huo pia aliendelea na ujenzi na ukarabati wa makanisa katika vigango vya Chitego,
Norini, Banyibanyi, Silale, Leganga, Chigwingwili, Songambele, Matongoro na Makawa.
Kila
mahali ambapo Mwenyezi Mungu amemjalia kukaa katika utume wake: yaani Mpwapwa, Kongwa,
Mlali, Mbuga na Mkoka aliwahudumia Taifa la Mungu na Jamii Kiroho na Kimwili (hasa
wakati wa njaa). Pia amebahatika kupokea watoto wachanga kwa ruhusa ya pekee ya Askofu
Mathias Isuja na kuishi nao misioni, kuwasomesha na kuwapatia mahitaji ya msingi
kwa maisha yao hadi kifo chake.
Lakini sio wao tu bali hata watoto wa wasaidizi
wake wa karibu katika kazi mbalimbali waliofariki na kuacha watoto wadogo amelazimika
kwa kuthamini majitoleo ya wazazi wao kuwatunza kwa kuwasomesha watoto hao wapatao
zaidi ya 40 kwa misaada ya Wafadhili. Anaeleza kwamba maisha ya watoto wa namna hii
yananigusa sana kwani hata yeye ni mtoto yatima ambaye alilelewa na Masista na Mapadre
mpaka amekuwa Kasisi na Mmisionari.
Mungu amemwita katika makao yake ya milele
akiwa na miaka 81 ya kuzaliwa, 64 ya Utawa, 56 ya Upadre na 51 ya Umisionari. Ndugu
Egidio alipenda sana kusimulia hadithi mbalimbali, na matukio mbalimbali ya maisha.
Alikuwa msimulizi wa kuvutia na asiyechoka na bila kuchosha. Pia, alikuwa mtu asiyepitwa
na wakati, alijiendeleza kwa kusoma na kutafuta habari mbalimbali za kidunia.
Lakini,
zaidi ya yote ndugu Egidio alikuwa mwenye moyo mkubwa, mwenye kujaa utu, mkarimu,
mpenda watu, mwenye huruma kwa waliohitaji. Mtu wa sala na ibada kubwa. Ni mtu aliyemtegemea
Mungu kwa karibu kila kitu. Hata siku anapelekwa hospitali, njiani alishauri gari
isimamishwe na kumwomba Padre mwenzake ampe huduma ya maungamo na mpako wa wagonjwa.
Ni kama alijua kifo chake kinakuja, kwa furaha aliwasalimia watu na kuagana kuwa hasa
wajitahidi katika kazi zao.
Alijitambulisha na kujifananisha na watu aliofanya
nao kazi. Hata siku za mwisho hakuona sababu tena ya kwenda likizo. Tunamshukuru Mungu
kwa zawadi ya Maisha yake na kumwombea Mungu ampokee kwenye uzima wa milele. Raha
ya Milele UmpeEe Bwana na Mwanga wa Milele Umwangazie – Apumzike kwa Amani – Amina.