2014-03-15 11:30:53

Padre Guidi Egidio amefariki dunia, mazishi yatafanyika tarehe 18 Machi 2014, Jimboni Dodoma


Mwanzilishi wa Parokia ya Mlali Jimbo Katoliki Dodoma Padre Guidi Egidio amefariki dunia Ijumaa, tarehe 14 Machi, 2014 majira ya saa tisa na nusu alasiri katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma. Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mkuu wa Shirika la Ndugu Wafransisco Wakapuchini Tanzania Padre Wolfgang Pisa imebainisha kuwa Padre Egidi alikuwa akisumbuliwa na maradhi ya mapafu.

Padre Pisa amesema kuwa ibada ya kumwombea Padre Egidi itafanyika katika Parokia ya Mtakatifu Yosefu Mchumba wa Bikira Maria Mkoka tarehe 17 Machi 2014 na kufuatiwa na mkesha Parokiani hapo. Amesema kuwa mazishi ya Padre Egidi yatafanyika tarehe 18 mwezi huu katika makaburi ya Shirika katika Parokia ya Kongwa saa tano kamili asubuhi.

Itakumbukwa kuwa Padre Egidi hadi mauti yanamfika alikuwa Paroko wa Parokia ya Mkoka na vile vile alikuwa mkurugenzi wa idara ya muziki Jimbo Katoliki Dodoma. Marehemu Padre Egidi alizaliwa tarehe 17.3.1933 nchini Italia na mara baada ya majiundo yake ya upadre alikwenda nchini Tanzania kunako mwaka 1963.

Padre Egidi katika utume wake amefanya kazi za utume katika Parokia za Kibakwe, Mpwapwa, Kongwa, Mlali na Mkoka. Padre Egidi amefariki akiwa na umri wa miaka 81, Raha ya milele umpe Ee Bwana na mwanga wa milele umwangazie. Apumzike kwa amani. Amina.








All the contents on this site are copyrighted ©.