2014-03-15 07:48:00

Kanisa litaendelea kutetea dhamana na utume wake katika sekta ya elimu


Baraza la Maaskofu Katoliki Italia linasema, Kanisa litaendelea kusimama kidete kulinda na kiutetea dhamana na utume wake katika sekta ya elimu, ili kuwajengea wanafunzi uwezo wa kukabiliana na changamoto za maisha kwa ujasiri mkubwa, huku wakizingatia maadili na utu wema. RealAudioMP3

Kwa kutambua dhamana hii, hapo tarehe 10 Mei 2014, Baraza la Maaskofu, Waamini, Wanafunzi, pamoja na watu wenye mapenzi mema, wataungana na Baba Mtakatifu Francisko kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro kutetea umuhimu wa elimu kwa vijana wa kizazi kipya. Lengo ni kulinda, kutetea na kuendeleza sekta ya elimu hasa wakati huu wa mtikisiko wa uchumi kimataifa unaopelekea Serikali kubana matumizi hata katika Sekta ya Elimu inayopaswa kupewa kipaumbele cha kwanza.

Hayo yamebainishwa hivi karibuni na Askofu Nunzio Galantino, Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Italia wakati alipokuwa anafafanua kuhsu utekelezaji wa mikakati ya Baraza la Maaskofu Katoliki Italia katika sekta ya elimu kwa kipindi cha Miaka kumi. Maaskofu wanasema kwamba, elimu ni kwa ajili ya mafao ya wengi na kwamba, malezi na majiundo ya binadamu ni muhimu sana kabla ya kuweka mbele faida na masilahi ya mtu binafsi au kikundi cha watu.

Shule ni mahali ambapo vijana wa kizazi kipya wanajenga na kudumisha misingi ya kijamii, kiutu na kiakili, kumbe, umuhimu wa shule makini ni jambo ambalo haliwezi kufumbiwa macho katika Jamii inayojikita katika maendeleo ya watu wake! Kanisa katika mikakati yake ya kichungaji, daima limekuwa likitoa kipaumbele cha pekee katika sekta ya elimu kwa kutambua umuhimu wa elimu katika majiundo ya mtu mzima: kiroho na kimwili; elimu inayomwezesha mwanadamu kuwa huru na mwenye ufahamu mpana katika kuchambua na kunyambulisha mambo, ili kujenga na kudumisha Jamii inayosimikwa katika ukweli, amani, haki na usawa.

Maaskofu wanatambua kwamba, athari za myumbo wa uchumi kimataifa zimewatumbukiza wananchi wengi wa Italia katika umaskini wa hali na kipato kiasi kwamba, kuna baadhi ya familia zinakosa mahitaji yake msingi, lakini shule zinapaswa kuthaminiwa na kupewa kipaumbele cha pekee katika sera na mikakati ya Serikali na wadau mbali mbali wa elimu nchini Italia. Hii ni sekta inayohitaji Serikali kujisadaka, kwa ajili ya mafao na ustawi wa demokrasia. Kuna haja pia kuweka uwiano mzuri kati ya kazi na elimu, ili kusaidia mchakato wa mabadiliko katika Jamii.

Askofu Nunzio Galantino, Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Italia anasema, juhudi zote hizi zinazofanywa na Kanisa Katoliki nchini Italia ni kwa ajili ya ustawi, maendeleo na mafao ya wengi.








All the contents on this site are copyrighted ©.