2014-03-15 09:13:46

Kanisa halina budi kushikamana na maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii


Baba Mtakatifu Francisko katika maadhimisho ya Kumbu kumbu ya Mwaka mmoja tangu alipochaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki, amebahatika kufanya mahojiano maalum na Kituo cha Radio cha Bajo Flores, FM 88.1 kinachorusha matangazo yake nchini Argentina. Haya ni mahojiano yaliyofanywa kwa njia ya Video, ambamo Baba Mtakatifu anakazia uwepo wa Kanisa miongoni mwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii ili waweze kuonja huruma na upendo wa Mungu.

Baba Mtakatifu anakazia umuhimu wa waamini kujitokeza kifua mbele kutangaza Injili ya Furaha hadi miisho ya dunia. Anawakumbuka kwa namna ya pekee, Mapadre, Watawa na Waamini walei wanaoendelea kushuhudia uwepo wa Kanisa kati ya Maskini kwa njia ya huduma makini huko Argentina. Huu ni utume ambao anaufahamu kwa kina kwani ulikuwa ni sehemu ya mikakati yake ya kichungaji alipokuwa Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Buenos Aires.

Baba Mtakatifu anakazia umuhimu wa huduma ya elimu makini kwa maskini, kama nyenzo msingi inayoweza kuwaletea ukombozi wa kweli dhidi ya ujinga na umaskini, tayari kupambana na mazingira katika maisha yao. Uwepo wa Mapadre na Watawa usaidie mchakato wa kuwasindikiza vijana katika makuzi na malezi makini kwani huu ni utume unaopewa kipaumbele na Mama Kanisa. Hawa ni viongozi wa Kanisa wanaotaka kujenga mshikamano wa upendo na maskini kwa kusimama kidete kulinda na kutetea haki zao msingi.

Baba Mtakatifu anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuguswa na mahangaiko ya jirani zao, tayari kushikamana kwa upendo katika huduma, kwani binadamu wanategemeana na kukamilishana, hakuna mtu anayeweza kujigamba kwamba, anajitosheleza kwa yote. Vyombo vya habari vijitahidi kutangaza na kueneza ukweli, kwa kutoa kipaumbele kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, kwani hata wao wanapaswa kusikika.

Baba Mtakatifu anasema kati ya mambo yanayompatia ugumu katika maisha na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro ni kukaa ofisini na kuanza kushughulikia makaratasi, ni jambo ambalo anasema limeendelea kumtesa katika maisha yake kama Askofu na sasa kama Papa. Anawaalika waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema kusali kwa ajili yake. Kwa kweli, watu kutoka sehemu mbali mbali za dunia wanaendelea kusali na kumwombea Baba Mtakatifu Francisko katika maisha na utume wake.







All the contents on this site are copyrighted ©.