2014-03-14 10:52:33

Watanzania wanaomboleza kifo cha Askofu mstaafu Lukanima


Rais Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia salamu za rambirambi Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania pamoja na Kardinali Polycarp Pengo, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dar es Salaam kufuatia kifo cha Askofu Mstaafu Fortunatus Lukanima aliyekuwa Askofu wa Jimbo Katoliki la Arusha anayetarajiwa kuzikwa Parokiani Kagunguri, Jimbo Katoliki la Bunda, Jumamosi, tarehe 15 Machi 2014.

“Kwa masikitiko makubwa napenda kutoa pole zangu za dhati kwa kuondokewa na kiongozi mahiri wa kidini katika jamii yetu” Rais amesema na kueleza kuwa si wakatoliki na familia yake tu ambao wameondokewa na mpendwa wao bali “ Kwa pamoja tumepoteza kiongozi wetu wa kiroho, mshauri mkubwa mwenye mapenzi na watu wake na nchi kwa ujumla” Rais ameongeza .

“Naungana nanyi nyote katika kipindi hiki kigumu cha majonzi, Familia ya Marehemu na jamii yote ambayo Marehemu Baba Askofu alitumikia kwa moyo wake wote kwa upendo mkubwa. Hatuna namna ya kufarijiana bali kwa pamoja kuungana na kumuombea Marehemu Baba Askofu mapumziko mema ya Milele” Rais amesema.

Rais ametuma rambirambi hizo mara baada ya kupokea taarifa rasmi kutoka Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) ambayo imemtaarifu kuhusu kifo hicho kilichotokewa tarehe 12 Mach katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando ambapo Marehemu alikua akipata matibabu.








All the contents on this site are copyrighted ©.