Watanzania wanaomboleza kifo cha Askofu mstaafu Lukanima
Rais Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia salamu za rambirambi Rais wa Baraza la Maaskofu
Katoliki Tanzania pamoja na Kardinali Polycarp Pengo, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la
Dar es Salaam kufuatia kifo cha Askofu Mstaafu Fortunatus Lukanima aliyekuwa Askofu
wa Jimbo Katoliki la Arusha anayetarajiwa kuzikwa Parokiani Kagunguri, Jimbo Katoliki
la Bunda, Jumamosi, tarehe 15 Machi 2014.
“Kwa masikitiko makubwa napenda kutoa
pole zangu za dhati kwa kuondokewa na kiongozi mahiri wa kidini katika jamii yetu”
Rais amesema na kueleza kuwa si wakatoliki na familia yake tu ambao wameondokewa na
mpendwa wao bali “ Kwa pamoja tumepoteza kiongozi wetu wa kiroho, mshauri mkubwa mwenye
mapenzi na watu wake na nchi kwa ujumla” Rais ameongeza .
“Naungana nanyi nyote
katika kipindi hiki kigumu cha majonzi, Familia ya Marehemu na jamii yote ambayo
Marehemu Baba Askofu alitumikia kwa moyo wake wote kwa upendo mkubwa. Hatuna namna
ya kufarijiana bali kwa pamoja kuungana na kumuombea Marehemu Baba Askofu mapumziko
mema ya Milele” Rais amesema.
Rais ametuma rambirambi hizo mara baada ya kupokea
taarifa rasmi kutoka Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) ambayo imemtaarifu
kuhusu kifo hicho kilichotokewa tarehe 12 Mach katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando
ambapo Marehemu alikua akipata matibabu.