2014-03-14 09:46:58

Jifungeni kibwebwe kulitegemeza Kanisa Barani Afrika!


Kanisa Barani Afrika halina budi kuhakikisha kwamba, linajifunga kibwebwe katika sera na mikakati yake ya kichungaji inayopania kulitegemeza Kanisa badala ya kuendelea kubweteka kwa kutegemea misaada kutoka ng'ambo jambo ambalo kwa sasa limepitwa na wakati. Haya ni kati ya mambo yaliyoibuliwa wakati wa Kongamano lililoandaliwa na Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika na Madagascar, SECAM, kwa ajili ya Makatibu wakuu wa Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Kikanda na Kitaifa huko Johanesburg, Afrika ya Kusini.

Hii ni changamoto iliyotolewa na Padre Nicholas Afriyie, Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Ghana wakati wa kuchangia katika mada kwenye Kongamano hilo. Umefika wakati kwa SECAM kuanzisha kitengo ambacho kitatafuta fedha kutoka Barani Afrika kwa ajili ya utekelezaji wa mikakati ya maendeleo na ustawi wa Familia ya Mungu Barani Afrika.

Kitengo hiki kinapaswa kutambua na kuonesha mahali ambapo Kanisa linaweza kupara rasilimali ya kugharimia miradi yake na uwezekano uliopo ndani ya Kanisa Barani Afrika. Waamini wakijizatiti inawezekana kabisa kulitegemeza Kanisa Barani Afrika, hasa kwa kuwahusisha waamini walei, kwa kuwa na nidhamu, ukweli na uwazi katika matumizi ya mali ya Kanisa.

Katika kongamano hili wajumbe pia wamefundishwa umuhimu na matumizi ya mitandao ya kijamii kwa ajili ya kuwatangazia watu Habari Njema ya Wokovu. Wajumbe wameweka mikakati na ratiba ya Maadhimisho ya Mwaka wa Upatanisho Barani Afrika, hapo mwakani baada ya kuthibitishwa na SECAM. Kongamano hili limewashirikisha viongozi wa Kanisa kutoka Afrika ya Kusini na wadau wengine wa SECAM katika utekelezaji wa miradi na mikakati ya SECAM Barani Afrika.







All the contents on this site are copyrighted ©.