2014-03-13 09:50:45

Yaliyojiri katika maisha na utume wa Papa Francisko


Kardinali Jorge Bergoglio aliyechagua jina la Mtakatifu Francisko wa Assisi, fukara, mpenda amani na mtunza mazingira ni Papa wa 265 aliyeuanza utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro kwa moyo wa unyenyekevu na unyofu wa kiinjili. Ni Papa wa kwanza kuchaguliwa kutoka katika Shirika la Wayesuit na Papa wa kwanza kutoka Kanisa la Amerika ya Kusini. RealAudioMP3

Papa Francisko katika mahubiri yake ya mwanzo kabisa, ameonesha mbinu mkakati wa shughuli za kichungaji kwa Kanisa ambalo linapaswa kutembea, kujenga na kushuhudia. Alipochaguliwa na Makardinali wenzake, aliambiwa kamwe asiwasahau wala kuwatelekeza maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii kutokana na hali yao n anafasi zao za maisha, ili kwamba wote wanaotafuta: maana, huruma na upendo wa Mungu katika maisha yao, waweze kuuonja kwa njia ya Mama Kanisa.

Baba Mtakatifu anakumbusha kwamba, dhamana ya uongozi ni huduma kwa Taifa la Mungu pasi na kumezwa na malimwengu. Huruma na upendo wa Mungu ambaye kamwe hachoki kusamehe na kusahau ni kati ya mambo makuu ambayo yameendelea kukaziwa na Baba Mtakatifu Francisko katika maisha na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, mwaka mmoja tangu achaguliwe kuliongoza Kanisa Katoliki. Haya ni mambo ambayo yameandikwa katika vinasaba vya maisha yake, kama inavyoonesha hata katika Nembo yake ya Kipapa. Anasema upendo wa Mungu una nguvu ya kufanya mabadiliko makubwa katika maisha ya mwanadamu. Kumbe, vijana wasikubali kamwe, kupokonywa matumaini ya maisha yao na wajanja wachache.

Baba Mtakatifu anawaalika viongozi wa Kanisa kutoka Sakristia na kuwaendelea watu mahali waliko, ili waweze kuwaonjeshe huruma na upendo wa Mungu kwa kuwatangazia Injili ya Furaha, huku wakikazia mambo msingi katika maisha.

Wachunguzi wa masuala ya historia ya Kanisa walikuwa wanajiuliza maswali yasiyokuwa na majibu. Je, inawezekanaje Kanisa kuwa na Mapapa mawili kwa mpigo? Baba Mtakatifu Francisko ameonesha kwamba, jambo hili linawezekana hata pengine si mara ya kwanza kuanzia sasa Kanisa likaweza kuwa na Papa mstaafu kama ilivyo kwa Papa mstaafu Benedikto wa kumi na sita ambaye amekuwa kweli ni hazina ya Kanisa, Kiongozi mnyofu na asiyependa makuu anayeutumia muda wake mwingi kwa ajili ya kutafakari Neno la Mungu na kuliombea Kanisa la Kristo.

Baba Mtakatifu Francisko anawataka viongozi wa Kanisa kujitosa kimasomaso kwa ajili ya kuwahudumia watu wa Mungu waliokabidhiwa kwao na Kanisa. Katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo, Kanisa halina budi kuwacha milango yake wazi kwa ajili ya wote wanaotafuta kukutana na kuzungumza na Kristo; wale wanaotaka kujipatanisha na Mungu pamoja na jirani zao; kwa wale wote wanaotaka kukumbatiwa na Mama Kanisa ili kuondokana na upweke hasi unaowaandama katika hija ya maisha yao.

Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kulichangamotisha Kanisa kujenga na kudumisha utamaduni wa kukutana na kujadiliana na watu kama sehemu ya vinasaba vya maisha na utume wake. Kanisa linatambua kwamba, lina dhamana ya kuganga na kuponya madonda mbali mbali yanayomwandama mwanadamu katika hija ya maisha yake hapa duniani.

Watu waguswe na mahangaiko ya jirani zao wanaoteseka kutokana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa, watu wasiokuwa na ajira; watu ambao wamekumbwa na maafa asilia; watu wanaotaka kusalimisha maisha yao kutokana na vita, dhuluma na nyanyaso za kidini na kikabila. Hili ni kundi la watu ambalo linapaswa kumegewa na kushirikishwa udugu na mshikamano unaojali. Kwa bahati mbaya anasema Baba Mtakatifu kuna watu ambao kwa sasa vita, maafa ya wakimbizi na wahamiaji huko Baharini si habari tena na wala hakuna anayetokwa na machozi kwa watu kama hawa kufariki dunia.

Baba Mtakatifu anasema anaendelea kutekeleza maamuzi yaliyotolewa kwenye Mabaraza ya Makardinali katika vikao vyao elekezi kabla ya uchaguzi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro: Kwanza kabisa mageuzi haya hayana budi kuanzia katika Sekretarieti ya Vatican, Benki ya Vatican pamoja na taasisi zote zinazoendeshwa na Vatican kwa kukazia: weledi na huduma; nidhamu, ukweli na uwazi, kanuni pamoja na sheria. Jambo la msingi ni toba na wongofu wa ndani.

Familia ni taasisi ambayo kwa sasa inapewa kipaumbele cha pekee na Baba Mtakatifu Francisko, ili kuhakikisha kwamba, inaweza kutekeleza utume na dhamana yake kadiri ya mpango wa Mungu kwa maisha ya mwanadamu. Waamini na watu wote wenye mapenzi mema wajitaabishe kuhakikisha kwamba, wanadumisha maagano ya Sakramenti ya Ndoa, pale ndoa inapovunjika, basi watu wasikitike, kwani changamoto kubwa ni kuchuchumilia utakatifu wa maisha ya ndoa na familia.

Haki na amani sehemu mbali mbali za dunia ni kati ya mambo ambayo Baba Mtakatifu anaendelea kuyafanyia kazi kwa sala na majadiliano ya kina, lakini zaidi kwa kuitaka Jumuiya ya Kimataifa kuwa makini na biashara ya silaha duniani inayoendelea kusababisha maafa makubwa kwa watu wasiokuwa na hatia. Baba Mtakatifu ni kati ya watu mashuhuri sana duniani, lakini anayepaswa kupewa sifa na utukufu ni Yesu Kristo Mkombozi wa ulimwengu. Kwa ufupi haya ni kati ya yale yaliyojiri katika maisha na utume wa Baba Mtakatifu Francisko, Mwaka mmoja tangu alipochaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki, tarehe 13 Machi 2013.

Imehaririwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.