2014-03-13 09:54:45

Watu wengi wameguswa na kuvutwa na unyofu wa Papa Francisko


Mwaka mmoja umegota tangu Papa Francisko alipochaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki. Watu wengi ndani na nje ya Kanisa wamevutwa na kuguswa na maisha, ujumbe na changamoto zinazoendelea kutolewa na Baba Mtakatifu Francisko wakati huu. RealAudioMP3

Ni ujumbe na changamoto zinazogusa undani wa maisha ya mtu kwani zimesheheni: upendo na huruma ya Mungu kwa watu wake. Ni kiongozi ambaye ameonesha ukaribu kwa watu maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Kwa maneno mengine, huu ni upendo wa Mungu unaogusa na kuponya.

Ni maneno ya Padre Federico Lombardi, msemaji mkuu wa Vatican na Mkurugenzi wa Radio Vatican, katika mahojiano maalum na Radio Vatican, wakati huu Mama Kanisa anapomwimbia Mwenyezi Mungu utenzi wa sifa na shukrani kwa ajili ya Papa Francisko, kutimiza mwaka mmoja tangu alipochaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki. Ni mwaka ambao umekuwa na pilika pilika nyingi, lakini kuna matukio ambayo bado yanaendelea kukumbukwa na wengi kwani yamenata katika mioyo ya watu kama nta safi. Moja kati ya matukio haya ni usiku ule alipoinamisha kichwa chake, kuomba sala kutoka kwa maelfu ya watu waliokuwa wamefurika kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican.

Padre Lombardi anakumbuka Alhamisi kuu jioni, alipowatembelea vijana waliokuwa gerezani na kuadhimisha Ibada ya Misa ya Alhamisi kuu kwa kuwaosha miguu, kielelezo cha huduma ya upendo kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Bado wengi wanamkumbuka Baba Mtakatifu alipofanya hija ya kichungaji Kisiwani Lampedusa mlango wa matumaini ya watu kutoka Barani Afrika wanaopania kuokoa na kuboresha maisha, wanapozama maji hata kabla ya kuwasili nchini Italia tayari kuelekea na safari zao sehemu mbali mbali za Bara la Ulaya.

Pengine maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013 yaliwagusa wengi kwani Baba Mtakatifu aliwapatia vijana changamoto ya kutoa kipaumbele cha pekee kwa Kristo na Kanisa lake, wawe ni wadau wa Uinjilishaji wa kina na wala si watazamaji wanaopunga upepo kutoka maghorofani!

Padre Lombardi anasema, Waraka wa Injili ya Furaha ni muhtasari wa mpango mkakati wa shughuli za kichungaji zinazopaswa kutekelezwa na Mama Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya Tatu ya Ukristo, kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa Familia ya Binadamu. Wazo hili linajieleza wazi kutokana na Mabaraza ya Makardinali yaliyofanyika Mwezi Februari 2014 kwa kuangalia changamoto za kichungaji zinazoikumba Familia katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia.

Padre Federico Lombardi anasema kwamba, Kanisa ni Familia ya Mungu inayofanya hija ya toba na wongofu wa ndani, tayari kujenga na kuimarisha Ufalme wa Mungu kwa njia ya ushuhuda wa imani tendaji; ikiwa tayari kutekeleza mapenzi ya Mungu katika maisha ya mwanadamu.

Baba Mtakatifu Francisko katika kipindi cha Mwaka mmoja wa uongozi wake, ameendelea kulichangamotisha Kanisa kufanya hija katika maisha na utume wake, kwa ajili ya mafao na maendeleo ya binadamu wote, lakini zaidi wale wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Viongozi wa Kanisa wawe makini kuonesha njia na dira kwa watu waliodhaminishwa kwao na Mama Kanisa, ili waweze kuona barabara inayowaelekeza kwa Kristo na Kanisa lake. Hii ndiyo hija inayofumbatwa katika Maadhimisho ya Sinodi mbali mbali zitakazoadhimishwa mjini Vatican, kama kielelezo cha umoja, upendo na mshikamano wa Kikanisa. Haya ni mang’amuzi ya kibinadamu na Kikristo.

Baba Mtakatifu Francisko ana mwono na mtazamo wa mbali unaogusa maisha ya watu ndani na nje ya Kanisa. Anamwangalia binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu; anayepaswa kuheshimiwa na kuthaminiwa tangu pale anapotungwa mimba tumboni mwa Mama yake. Huu ndio ujumbe ambao Baba Mtakatifu anapenda kuwashirikisha Wakuu wa Mataifa, Taasisi na vyombo vya habari wanapokutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu.

Kila mwamini anashirikishwa katika maisha na utume wa Kanisa. Padre Lombardi anasema, picha kubwa ambazo bado zinaendelea kuzunguka kichwani pake ni kuona umati mkubwa wa watu wanaofurika kila Jumatano na Jumapili kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican walau kumwona, kumsikiliza na kuzungumza naye. Baba Mtakatifu kila mara anapohitimisha Katekesi yake, watu wa kwanza kusalimiwa ni wagonjwa ambao hata katika mateso na mahangaiko yao, wanapendwa na kuthaminiwa na Kanisa. Wagonjwa na maskini ni watu ambao daima wamekuwa na upendeleo wa pekee kutoka katika Injili, jambo linalooneshwa pian a Baba Mtakatifu Francisko kwa sasa.

Katika sakata la habari kutoka mjini Vatican, mdau mkuu ni Baba Mtakatifu Francisko mwenyewe anasema Padre Lombardi ambaye ndiye msemaji wake mkuu. Baba Mtakatifu ana uwezo wa kuwafikia watu moja kwa moja bila hata ya kuhitaji huduma ya Msemaji mkuu wa Vatican, jambo ambalo Padre Lombardi anasema, linamfurahisha sana. Ujumbe wa Baba Mtakatifu unapaswa kuwafikia na kuwagusa watu moja kwa moja katika undani wao!

Imehaririwa na
Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.