2014-03-12 07:49:34

Tokeni kifua mbele kutangaza Injili ya Furaha!


Wakristo wanachangamotishwa na Mama Kanisa kujitokeza kifua mbele kuwatangazia watu Injili ya Furaha na kuwaonjesha ushuhuda wa imani tendaji inayofumbatwa katika Neno la Mungu na maisha ya Kisakramenti. Kuna maelfu ya wakristo ambao wamesahau Mlango wa Kanisa, hawa wanapaswa kuoneshwa ushuhuda wa maisha ya Kikristo yenye mvuto na mashiko. RealAudioMP3

Wakati wa kupepeta mdomo umekwisha, watu wanataka kuona Injili ikilimwilisha katika uhalisia wa maisha ya watu, vinginevyo watu wataendelea kuogelea katika utupu na mkanganyiko wa maisha. Wakristo wajitokeze kushiriki kikamilifu katika mchakato wa Uinjilishaji Mpya unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili, kwa kuwashirikisha watu Injili ya Furaha inayobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake.

Hii ni changamoto ambayo imetolewa hivi karibuni na Kardinali Antonio Canizares Llovera, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Ibada na nidhamu ya Sakramenti, wakati wa Ibada ya Misa Takatifu kuhitimisha Jubilee ya Miaka 100 tangu Jimbo la Bikira Maria wa Antiqua lilipoanzishwa. Itakumbukwa kwamba, hili ni Jimbo la kwanza kabisa kuanzishwa Amerika ya Kusini.

Kardinali Canizares Llovera alikuwa anamwakilisha Baba Mtakatifu Francisko katika kufunga Jubilee hii ambayo ilizinduliwa Mwezi Septemba 2012, kwa mwaliko wa kumwilisha Injili ya Furaha katika vipaumbele vya maisha ya waamini, kama kielelezo cha ushuhuda wa imani tendaji. Waamini hawana sababu ya msingi ya kuogopa “kujimwaga duniani” kwa ajili ya kutangaza na kushuhudia Injili ya Furaha, huku wakiendelea kuwamegea jirani zao upendo unaobubujika kutoka kwa Kristo na Kanisa lake.

Waamini wawe ni watu wenye uwezo wa kupokea na kutoa msamaha kwa wale wanaowakosea, dhamana ambayo kimsingi si lele mama kutokana na ukweli kwamba, watu wengi wanapenda kulipiza kisasi. Wakristo wawe ni chombo cha upendo kwa watu wanaoteseka kutoka na umaskini, ujinga na maradhi. Wawe ni kielelezo cha matumaini ya watu waliokata tamaa kutokana na umaskini wa kiroho, unaotaka kumng’oa Mungu kutoka katika undani wa maisha na mikakati yao.

Kardinali Canizares Llovera anawaonya waamini kutoyakumbatia malimwengu, bali wawe ni chumvi na mwanga wa kuyatakatifuza, kwa kuonesha ukomavu katika uhuru na ushuhuda wa imani tendaji. Hapa hakuna Injili Mpya inayotangazwa, bali ni umwilishaji wa Neno la Mungu ili kuyachachua malimwengu kwa njia ya ushuhuda wa maisha yanayojikita katika imani kwa Kristo na Kanisa lake. Kardinali Antonio Canizares Llovera anahitimisha mahubiri yake kwa kuwaweka Wakristo wote wa Panama chini ya ulinzi na usimamizi wa Bikira Maria, msimamizi wao, ili awasaidie kuwa kweli ni cheche za matumaini kwa Familia na kwa nchi ya Panama katika ujumla wake.








All the contents on this site are copyrighted ©.