2014-03-11 09:06:51

Mshikamano na umoja wa kitaifa ili kupambana na changamoto mbali mbali nchini Togo!


Baraza la Maaskofu Katoliki Togo katika ujumbe wake mara baada ya maadhimisho ya mkutano wake mkuu linasema kwamba, mapendekezo yaliyotolewa na Tume ya Ukweli, Haki na Amani, kuhusu mchakato wa uchaguzi mkuu na mabadiliko msingi yanayopaswa kufanywa kwenye Serikali pamoja na taasisi zake, yanaweza kuchangia kwa kiasi kikubwa kuimarisha msingi ya haki na amani; utawala bora unaozingatia sheria pamoja na kukoleza maendeleo na mafao ya wengi.

Maaskofu Katoliki nchini Togo pamoja na mambo mengine wamejielekeza zaidi katika masuala nyeti na changamoto zinazoendelea kuwaandama wananchi wa Togo katika ujumla wao. Maaskofu wanaitaka Serikali, vyama vya kisiasa na wadau wengine kujikita katika mchakato wa upatanisho, haki na amani ambao umezinduliwa hivi karibuni nchini humo.

Maaskofu wamejadili pia umuhimu wa majiundo makini na endelevu kwa ajili ya Mapadre na Watawa nchini Togo, bila kusahau kuwajengea uwezo walei na wanasiasa ili kutekeleza wajibu wao msingi katika maendeleo na ustawi wa wananchi wa Togo.

Baraza la Maaskofu limeangalia pia maisha na utume wa Kanisa Katoliki nchini Togo, ambalo waamini wake ni zaidi ya asilimia ishirini ya idadi yote ya wananchi wa Togo. Maaskofu wanajiandaa kwa ajili ya kushiriki kikamilifu katika matukio mbali mbali ya maisha ya Kanisa la Kiulimwengu na kwa namna ya pekee, sherehe za kuwatangaza Wenyeheri Yohane wa XXIII na Yohane Paulo II kuwa ni watakatifu hapo tarehe 27 Aprili 2014.

Maaskofu wamegusia mikakati ya shughuli za kichungaji kwa ajili ya huduma, majiundo awali na endelevu, mafundisho ya dini shuleni, hija za maisha ya kiroho ndani na nje ya Togo pamoja na kufanya mabadiliko katika Mahakama ya Kanisa Katoliki nchini kwa kuangalia kwa makini masuala ya kijamii na kisiasa nchini humo. Ni jukumu la wananchi wa Togo kushikimana na kujenga utawala wa sheria unaozingatia haki msingi za binadamu, umoja wa kitaifa, upatanisho na maendeleo endelevu.

Baraza la Maaskofu Katoliki Togo limeweka Mpango wa shughuli za kichungaji mwa kipindi cha Miaka mitatu, kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa maskini na wote wanaosukimizwa pembezoni mwa Jamii. Itakumbukwa kwamba, kunako miaka 1990 Togo ilijikuta inatumbukia katika mgogoro wa kisiasa na kiuchumi, hali iliyopelekea wananchi wengi kutumbukia katika umaskini wa hali na kipato. Hadi sasa kuna idadi kubwa ya wananchi wa Togo wanaishi chini ya kiwango cha umaskini duniani.







All the contents on this site are copyrighted ©.