Mali ya watawa ni kwa ajili Unjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho
na kimwili!
Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume hayana budi kuhakikisha kwamba, yanatumia vyema
mali ya Kanisa kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa katika maeneo yao, huku
wakisukumwa na fadhila ya huduma ya upendo kwa wale wanaowahudumia. Hii ni huduma
ya upendo inayodhihirisha imani tendaji katika maisha ya watu.
Ni sehemu ya
mahubiri yaliyotolewa na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican wakati wa
Ibada ya Masifu ya Jioni kwa ajili ya watawa waliokuwa wanashiriki katika semina maalum
kwa ajili ya wasarifu wa Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume. Semina hii ya kimataifa
ya siku tatu ilikuwa imeandaliwa na Baraza la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi
za Kitume na ilifanyika kwenye Chuo Kikuu cha Kipapa cha Mtakatifu Antoni kilichopo
mjini Roma. Watawa wamekumbushwa kwamba mali waliyo nayo ni kwa ajili ya huduma kwa
binadamu na utume wa Kanisa.
Kardinali Parolin anasema, Yesu alipokuwa anajaribiwa
Jangwani alimwambia Shetani kwamba, mtu hataishi kwa mkate peke yake bali kwa kila
neno linalotoka kinywani mwa Bwana. Huu ni mwaliko kwa watawa kuhakikisha kwamba,
wanatumia vyema rasilimali na mali waliyokabidhiwa na Mwenyezi Mungu kwa hekima na
busara; katika ukweli na uwazi; huku wakiwajibika barabara. Mashauri ya Kiinjili yajidhihirishe
wazi katika matumizi bora ya mali zinazomilikiwa na watawa pamoja na kupambanua kikamilifu
vipaumbele vya matumizi ya mali hii.
Wakati huu wa athari za myumbo wa uchumi
kimataifa, kuna haja kwa watawa kujifunga kibwebwe kuhakikisha kwamba, karama ya mashirika
yao inakuwa ni kigezo msingi katika kuchagua vipaumbele vya matumizi ya mali ya Mashirika
ya Kitawa. Wachunguze kwa umakini mkubwa wapi ambapo kumekuwepo na uzembe kiasi kwamba,
Mashirika haya yamepoteza mali ya Kanisa au mali hii imetumika kinyume cha taratibu
na kanuni za Shirika husika.
Kardinali Parolin anasema, inasikitisha kuona
kwamba, athari za myumbo wa uchumi kimataifa zinaathiri hata utendaji wa shughuli
za huduma msingi kwa Jamii katika nchi za Kimissionari. Ili kukabiliana na changamoto
hizi zote, watawa wanapaswa kuhakikisha kwamba, wanaongozwa vyema na Neno la Mungu
linalomwilishwa katika karama na moyo wa Shirika katika utimilifu wake.
Wasi
wasi wa athari za myumbo wa uchumi kimataifa zisiwafanye watawa kutowashirikisha wengine
huduma ya upendo kwa kama walivyohofia Mitume walipokuwa kule Jangwani wakajikuta
wakiwa na Samaki watano na Mikate miwili, lakini Yesu kwa njia ya ukarimu huu aliweza
kuwalisha watu zaidi ya elfu tano kama inavyosimuliwa katika Injili.
Mashirika
ya kitawa yajifunze kubana matumizi, lakini yawe pia na mbinu na mikakati ya matumizi
bora ya mali ya Shirika. Watu wanaokabidhiwa kutunza fedha na mali ya Shirika waandaliwe
vyema, kwa kutambua kwamba, mali hii ni kwa ajili ya huduma ya Kiinjili inayomwilishwa
katika upendo kwa ajili ya Mungu na mwanadamu. Watawa wakiweza kudhibiti matumizi
ya fedha na mali ya Mashirika yao kwa ajili ya huduma kwa Kanisa, wataweza kushangaa
kuona kwamba, fedha na mali hiyo inaongezeka maradufu.
Hakuna muujiza ambao
Mwenyezi Mungu anaweza kuufanya kwa kuongeza fedha na mali ya Mashirika ya Kitawa,
lakini jambo la msingi ni kuhakikisha kuwa, wanatumia vyema fedha na mali ya Mashirika
kwa malengo yaliyowekwa mintarafu karama ya Shirika husika, huku wakiendelea kuwa
na matumaini kwa Mwenyezi Mungu badala ya kujikatia tamaa na kujifunga katika ubinfasi
na uchoyo wao.
Kardinali Parolin anawaambia Watawa kujitahidi kwanza kuutafuta
Ufalme wa Mungu na mengineyo watayapata kwa ziada. Kwa kuwa na matumizi bora ya rasilimali
na mali ya Mashirika ya Kitawa, kazi ya Uinjilishaji Mpya itasonga mbele.
Akichangia
mada kwenye semina hii ya kimataifa, Kardinali Joao Braz de Avis, Mwenyekiti wa Baraza
la Kipapa la Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume amewataka watawa kuwa na matumizi
bora na sahihi ya mali ya Mashirika. Viongozi wa Mashirika wamepewa dhamana na Kanisa
kusimamia na kuratibu mali ya Mashirika kwa kusaidiana na Wasarifu wao.
Kumbe,
kuna haja ya kuhakikisha kwamba, matumizi ya mali na fedha za Mashirika ya Kitawa
yanafuata Sheria na Kanuni za Kanisa na Mashirika husika, ili kudhibiti ubadhirifu
unaoweza kufanywa na baadhi ya watawa wanaoweza kumezwa na malimwengu na hivyo kusababisha
kashfa kama ambavyo zimewahi kujitokeza ndani ya Kanisa sehemu mbali mbali za dunia.
Mali ya Kanisa inapaswa kudhibitiwa na Sheria pamoja Kanuni za Kanisa pamoja na Sheria
za nchi husika.
Washiriki wa semina hii ya kimataifa wamegusia pia matatizo
na changamoto wanazokabiliana nazo katika utekelezaji wa mikakati mbali mbali ya kichungaji
kwa ajili ya Uinjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili.
Kimsingi, imesisitiziwa kwamba, Sheria, Kanuni na Katiba za Mashirika katika matumizi
ya mali za Kanisa zinapaswa kufuatwa kikamilifu bila kupuuziwa hata kidogo.