2014-03-11 08:59:26

Mafungo ni kipindi cha kufungua moyo ili kumsikiliza Roho Mtakatifu


Utakaso wa roho ndiyo kauli mbiu inayoongoza Mafungo ya kiroho ya Baba Mtakatifu Francisko pamoja na wasaidizi wake wa karibu yaliyoanza tangu Jumapili jioni huko Ariccia, nje kidogo ya mji wa Roma. Mafungo haya yanaongoza na Monsinyo Angelo De Donatis, Paroko wa Parokia ya Mwinjili Marko, Jimbo kuu la Roma.

Baba Mtakatifu wameendelea kushiriki kikamilifu katika Ibada ya Misa Takatifu, Tafakari na Ibada ya Kuabudu Ekaristi Takatifu. Monsinyo De Donatis katika tafakari yake anaendelea kukazia umuhimu wa mafungo katika maisha ya mwamini, changamoto kwao ni kujifunua kwa Roho Mtakatifu, ili kuimarisha maisha ya kiroho yanayowasaidia kukutana na Mwenyezi Mungu katika hija ya maisha yao ya ndani, wakiwa na mwanga mpya unaotoka kwa Mwenyezi Mungu.

Mafungo haya yawasaidie kukuza moyo wa: Sala, Ibada na Majitoleo kwa Mwenyezi Mungu pamoja na Kanisa lake. Ni wajibu wa waamini kutambua uwepo wa Mungu katika kazi ya uumbaji, bila ya kumwogopa. Itakumbukwa kwamba, wakati fulani katika maisha yao, mitume walishikwa na woga, kwa sababu hawakuwa na imani thabiti. Hali hii inaweza kumkuta mwamini ikiwa kama hawezi kuzamisha uhusiano wake wa dhati na Yesu Kristo na kusahau kwamba, Mwenyezi Mungu ni mwingi wa huruma na mapendo kwa waja wake.

Ukosefu wa imani anasema Monsinyo De Donatis kwamba, waamini wanajikuta wakiogelea katika maisha ya kinafiki na kutokujali, hali inayomfanya mhusika kutoa amri bila ya yeye mwenyewe kujihusisha katika utekelezaji wake. Ni watu wanaotaka kuwabebesha wengine mizigo mizito bila yao wao wenyewe kushiriki.

Kumbe, kuna haja kwa waamini kuhakikisha kwamba, wanasafisha roho zao ili kuondokana na picha hasi ya uwepo wa Mungu katika maisha yao, ili kuanza mchakato wa maisha ya kweli na matakatifu pasi na mawaa!







All the contents on this site are copyrighted ©.