2014-03-10 09:33:13

Sala Maalum kwa ajili ya Kuombea Bunge Maalum la Katiba Tanzania


Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania anawaalika waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema kusali kwa ajili ya kuombea Bunge Maalum la Katiba linaloendelea na vikao vyake mjini Dodoma. Ifuatayo ni sala unayoweza pia kuwashirikisha jirani zako:

Bwana Yesu,
Ulizaliwa Pangoni Bethlehem wakati Yosefu na Maria walipokwenda kusajili majina yao kwenye kitabu cha orodha ya raia. Nawe unaelewa umuhimu wa uongozi na utawala bora wa kiraia.

Nasi, wananchi wa Tanzania, sasa tupo katika kipindi muhimu kwa historia yetu. Wakati huu tunatafuta kwa pamoja namna ya kuendesha jamii yetu na kuweza kuboresha miundo yetu na taratibu zetu. Ee Bwana Yesu tunaomba msaada wako.

Utujalie mwanga wa Roho Mtakatifu na uvuvio wake, ili tuweze kutumia busara na hekima katika kutafuta yaliyo mema kwa taifa letu na mustakabali wake. Kwa namna ya pekee tunakuomba waangazie na kuwapa hekima wajumbe wote wa Bunge Maalum la Katiba, ili mioyo yao ijazwe upendo wako ulio nao kwa Taifa letu na watu wake. Tunawaombea waweze kuepuka kufanya kazi hiyo kwa kuongozwa na maslahi binafsi ama kutawaliwa na mawazo finyu ambayo ni kwa maslahi ya kisiasa tu.

Tunakusihi, tawala mioyo yao wakati wote wa mijadala wazingatie yaliyo mema kwa nchi yetu na watu wake.

Kwa Maombezi ya Bikira Maria, tunakuomba utongoze katika wakati huu muhimu kwa nchi yetu. AMINA.

Sala hii imetiwa sahihi na Askofu Tarcisius J. M. Ngalalekumtwa,
Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania na Askofu wa Jimbo Katoliki la Iringa
Tarehe 02. 03. 2014.







All the contents on this site are copyrighted ©.