2014-03-10 10:15:53

Jengeni umoja na mshikamano wa upendo!


Kardinali Chibly Langlois wa Jimbo Katoliki la Les Cayes, kutoka Haiti aliyeteuliwa na kusimikwa hivi karibuni wakati wa Maadhimisho ya Siku kuu ya Ukulu wa Mtakatifu Petro, Jumapili tarehe 9 Machi 2014 ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu ili kumshukuru Mungu kwa kuteuliwa kuwa ni Kardinali wa kwanza kutoka Haiti, changamoto ya kuonesha mshikamano wa umoja, upendo na udugu kwa wote.

Waamini wa Kanisa Katoliki nchini Haiti wametumia fursa hii kwa ajili ya kumwombea Baba Mtakatifu Francisko, amani, utulivu na upendo wakati huu anapoadhimisha Kumbu kumbu ya mwaka mmoja tangu alipochaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Kardinali Langlois katika mahubiri yake kwenye Ibada ya Misa Takatifu iliyodumu kwa takribani masaa matatu, amewataka wananchi wa Haiti katika ujumla wao, kujenga na kuimarisha mshikamano wa upendo ili kuwasaidia wale ambao wanaendelea kuteseka kutokana na baa la njaa, umaskini na ujinga nchini Haiti. Watoto wengi wameweza kwenda shule, kupata chakula na makazi bora kutokana na mchango wa Wasamaria wema.

Huu ni mwaliko kwa wananchi wote wa Haiti kushikamana kidugu ili kusaidiana kupambana na changamoto za maisha ya kila siku. Waamini na wananchi katika ujumla wao, wawe na ujasiri wa kushirikisha hata kile kidogo walicho nacho kwa ajili ya mafao ya wengi.

Kardinali Chibly Langlois mwenye umri wa miaka 55 ambaye ni kati ya Makardinali wenye umri mdogo kwenye Baraza la Makardinali anaonesha jinsi ambavyo Baba Mtakatifu Francisko anavyowathamini na kuwajali watu wanyonge, ili waweze kuondokana na unyonge wao, tayari kutoka kifua mbele kuwatangazia jirani zao Injili ya Furaha. Hata maskini katika umaskini wake, bado ni sehemu muhimu sana katika maisha na utume wa Kanisa. Kanisa linataka kuwahudumia maskini kwa ari na moyo mkuu kama anavyoonesha Baba Mtakatifu Francisko katika maisha na vipaumbele vyake.

Kardinali Langlois katika mahubiri yake amekazia pia umuhimu wa wananchi wa Haiti kushikamana kwa dhati, ili kujenga na kuimarisha umoja wa kitaifa. Ibada hii ya Misa Takatifu imehudhuriwa pia na watu wa dini na madhehebu mbali mbali nchini Haiti kwa kutambua kwamba, Kardinali Chibly Langlois ameteuliwa si tu kwa ajili ya Kanisa Katoliki nchini Haiti, bali ni daraja la upendo kwa watu wote.

Ibada hii ya Misa Takatifu imeadhimishwa kwenye Uwanja wa michezo wa Port - au Prince- kwani Kanisa kuu la Jimbo kuu la Port- au- Prince lilibomoka wakati wa tetemeko la ardhi lililoikumba Haiti kunako Mwaka 2010 na bado halijaanza kujengwa tena.







All the contents on this site are copyrighted ©.