Kardinali Osca Rodriguez Maradiaga, Rais wa Shirikisho la Mashirika ya Misaada ya
Kanisa Katoliki Kimataifa anasema, Siku ya Wanawake Duniani kwa Mwaka 2014 inalenga
kutambua uwezo wa wanawake katika mchakato wa maendeleo endelevu sanjari na kutafuta
suluhu ya ukosefu wa uhakika wa usalama wa chakula duniani. Wanawake sehemu mbali
mbali za dunia wamekuwa mstari wa mbele katika kuchangia mustakabali wa maendeleo
ya familia na jamii zinazowazunguka.
Wanawake wakiwezeshwa wanaweza kuchangia
katika maendeleo endelevu ya Jumuiya ya Kimataifa. Caritas Internationalis kwa kushirikiana
na Mfuko wa Fidel Gotz, katika Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani, watatoa jumla
ya Euro elfu kumi kwa makundi mawili: Kundi la kwanza ni lile linalotekeleza miradi
inayofadhiliwa na Caritas Internationali na sehemu ya pili, Mashirika mengine ya misaada
yanayojipambanua kwa kuwajengea uwezo wanawake uwezo kiuchumi. Tuzo hii itatolewa
hapo tarehe 16 Oktoba 2014 wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Chakula Duniani.