2014-03-07 08:14:30

Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya kwanza ya Kipindi cha Kwaresima


Mpendwa msikilizaji, leo tunatafakari masomo Dominika ya kwanza ya Kwaresima, kipindi cha mfungo mtakatifu. Kipindi ambacho cha kusali, kufunga na kupigana na mwovu shetani. RealAudioMP3

Kwa sala tunamwomba Mungu ujasiri wa kubadili maisha yetu ili tuambatane na Injili. Kwa kupigana na mwovu mkristu ataka kutawala hisia na vionjo vinavyokuza ubinafsi. Kwa kufunga mkristu hujikusanyia siraha, kwa ajili ya mapambano na hivi katika kufunga huweza kujitoa kuacha vitu ambavyo anaviona ni vya maana na hivi kwa kwa ajili ya kuwasaidia maskini. Kwa kuwasaidia wengine mkristu hujichagulia umaskini wa roho na hapa ndipo kuna kufunga kwa uhakika. Neno la Mungu Dominika ya kwanza ya Kipindi cha Kwaresima latualika kutafakari juu ya MAJARIBU (vishawishi).

Katika somo la kwanza toka kitabu cha Mwanzo tunapata simulizi juu ya Adamu na Eva wanaoishi katika bustani iliyojaa matunda na uzuri wa kila aina. Katikati ya bustani hii kuna mti maalum wa matunda ambao ndugu hawa hawakuruhusiwa kuugusa, kwa maana ulitengwa kwa ajili ya Mungu tu. Mti huu kwa hakika si rahisi kujua ni mti wa matunda yapi, lakini kwa hakika mwandishi ataka kuwasilisha mbele yetu “mti wa mema na mabaya”. Ni alama inayowakilisha zuio au mipaka ya utendaji wa mwanadamu.

Ni kwa jinsi hii tunatambua kuwa Mungu alimwumba mtu akiwa huru lakini ndani ya mipaka ya uwezo wake, yaani juu ya wema na ubaya hakuwa na nguvu ya kudai au kuamua! Ni Mungu pekee mwenye uwezo wa kupambanua wema na ubaya. Ni katika mantiki hii basi Mwanadamu alipotaka kwa kiburi chake kutambua wema na ubaya, akaangukia katika shimo la uharibifu. Hakuweza kuwa sawa na Mungu kama alivyofikiria bali ndo akawa amepoteza hata kile alichokuwa nacho!, akawa ameangukia katika kutawaliwa na vionjo na hisia zake na hivi hata kuweza kuchanganya mambo yaani kibaya anakiona chema na chema anakiona kibaya! Hali hii ipo leo katikati yetu au hakuna)? Tutafakari maisha yetu ya sasa!

Mpendwa msikilizaji tumeona sura ya mwanadamu ilivyokuwa na ilivyogeuka baada ya majaribu na kuwa saliti, inatupeleka kuona sura ya Bwana wa Agano jipya ilivyokuwa kabla ya vishawishi na baada ya vishawishi na hasa alivyovumilia na kushinda na hivi akatimiza mapenzi ya Mungu, kwa ajili ya wokovu wetu. Yafaa sasa kuona sura ya nyoka, tukijiuliza hivi mwandishi ataka kusema nini? Nyoka awakilisha kishawishi na kishawishi ni kutengana na Mungu. Ni kujikomaza katika ubinafsi na kumweka Muumba wangu pembeni kana kwamba naweza kuongoza maisha yangu mwenyewe!

Kishawishi huingia polepole na kwa siri katika moyo wa mtu kama nyoka alivyojipenyeza katika maisha ya Adamu na Eva. Uzuri wa mti wa matunda ulianza kujipenyeza katika hisia zao baada ya kushtuliwa na nyoka! Kwa hakika haikuwa rahisi kuchomoka kwa sababu tayari kiburi na majigambo yalikuwa yamekwishaingia moyoni mwao.

Mpendwa msikilizaji, kwa kumwacha Muumba mtu hujishusha toka hadhi yake ya mwanzo yaani hali ya kuwa huru na huanza kujisikia na kujiona uchi, na kwa namna hii hurudia hali ya kuwa kama mnyama ambaye hana cha kujisetiri! Mtu kwa kumwacha Mungu huingia katika laana na hivi chanzo cha vita, magomvi, wivu, ufisadi na mambo kama hayo. Kwa hakika laana hii imejifungamanisha katika dhambi na si kwamba Mungu huacha kumpenda mwanadamu. Ndiyo kusema kwa kutenda dhambi mtu hujiadhibu mwenyewe, huharibu ndoa yake, huharibu masomo yake, kazi yake na urafiki nk.

Mpendwa msikilizaji Neno la Bwana halituambii kilichotokea tu mwanzoni bali kile kinachotokea hivi leo katika maisha yetu ya kila siku. Kwa kuweka pembeni Neno la Mungu maana yake tunatangaza kupotea toka njia mapendo na ya uhuru na kuingia katika upotevu na uharibifu wa maisha yetu.

Mpendwa mwana wa Mungu, Mt Paulo anapowaandikia Warumi anaonesha waziwazi tofauti kati ya Adamu na Kristu Masiha. Adamu kwa kukosa utii kwa Mungu anapoteza uhuru wake na kuzama katika taabu na badala yake Kristu anamtii Baba yake na kwa njia hiyo ya utii mkamilifu anakuwa mfalme wa maisha na mwokozi wa Adamu na watu wote kwa ujumla. Sisi tunataka nini? maisha au taabu! Kama ni maisha basi utii ndiyo njia pekee katika kwaresima hii kuelekea uhuru kamili kama alivyokusudia Mwenyezi Mungu tangu mwanzo kabla ya anguko.

Katika somo la Injili tunapata kumwona Bwana ambaye anabaki mwaminifu kwa Baba yake, mbele ya majaribu, mbele ya shetani ambaye alitaka kumtoa katika msimamo wake wa kitume. Majaribu kwa Bwana yalikuwa daima mbele yake katika kipindi chote cha uchungaji. Kumbuka pale mwishoni mwa safari yake aliposema “Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha?” Ndiyo kusema majaribu tunayoyasikia katika Dominika hii ni ufupisho wa majaribu yote ambayo Bwana ameyapitia na akashinda!

Mwinjili Matayo ataka kutukumbusha kwa njia ya majaribu haya matatu, yale majaribu kwa Waisraeli huko jangwani tokea Misri. Jaribu I lahusu mkate na katika hili Bwana anapelekwa jangwani kama Waisraeli na anakaa huko siku 40 kama Waisraeli walivyokaa miaka 40 jangwani. Bwana anakemea jaribu hilo akisema mtu hataishi kwa mkate bali kwa kila Neno litokalo katika kinywa cha Mungu. Anasisitiza mambo ya kiroho kama njia ya wokovu na ataka kusema kwamba mali haitoshi bali muhimu amani na upendo katika maisha yetu. Fikiria mtu mmoja ana magari na mijumba ya kutosha lakini nyumbani ugomvi kila siku, kuna furaha katika mali ile? Tafakari!

Mpendwa, jaribu II lahusu hakikisho la kuwa kweli Mwana wa Mungu. Katika hili kumbukeni Waisraeli walipokuwa jangwani walimjaribu Bwana akawape maji toka katika mwamba! Na kwa namna haiyo walitaka kuhakikisha uwepo wa Mungu na upendo wake kwao! Kinyume cha fikra hizi Bwana anakataa kuomba ishara, hahitaji kuhakikisha upendo wa Mungu kwake maana upo na inaeleweka. Katika siku zetu hizi kuna kishawishi cha kutaka kuhakiki upendo wa Mungu kwetu, mfano mmoja anasema “Mungu kama wanipenda naomba nipate kazi!! Na pengine asipopata anaanza malalamiko. Hatupaswi kuomba namna hii bali kwa matumaini na hivi mapenzi yake yatimizwe.

Mpendwa jaribu la III lahusu madaraka na miliki za ulimwengu. Katika hili Waisraeli walipokuwa jangwani, walionekana kwa wakati fulani kumchoka Mungu wao na hivi wakaanza kujitengenezea visanamu na kuviabudu. Bwana akitambua hatari hii anakataa kabisa kuabudu vijisanamu vya kujitengenezea, anakataa kabisa kuiabudu siasa, fedha, mafanikio na nguvu za kivita bali anabaki mwaminifu kwa Baba yake. Kwa wakati wake walitarajia Masiha mwenye nguvu lakini Bwana anajitokeza kinyume chake na kuonesha unyenyekevu upeo na hasa akitaka kuwashirikisha uhuru walio maskini na wenye dhambi.

Mpendwa msikilizaji, Bwana anashinda mambo haya yote na hii ndiyo kwaresima kwake, ndiyo kwaresima yetu tunapoelekea katika heri ya milele. Tunapaswa kubaini daima mitego ya mwovu na kuweza kupambana nayo kwa ujasiri tukitumia siraha ndilo Neno la Mungu.
Mpendwa ninakutakia furaha na matumaini katika maisha yako daima ukimtanguliza Mungu na kwa namna hiyo kuijua hekima ya kweli ijengayo nguvu ya kushinda majaribu dhidi yako. Tumsifu Yesu Kristo.
Tafakari hii imeletwa kwako na Pd Richard Tiganya C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.