2014-03-07 10:02:56

Siku ya Wanawake Duniani, 8 Machi 2014


Mchakato wa mapambano dhidi ya baa la njaa duniani unaweza kupata mafanikio makubwa kwa kuwajengea wanawake uwezo kwa njia ya elimu makini ili waweze kushiriki kikamilifu katika uzalishaji kwenye sekta ya kilimo.

Shirika la Mpango wa Chakula la Umoja wa Mataifa katika Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani inayoadhimishwa tarehe 8 Machi, 2014 linaitaka Jumuiya ya Kimataifa kuwajengea uwezo wanawake ili kupambana kikamilifu na ukosefu wa uhakika wa usalama wa chakula pamoja na utapiamlo unaoendelea kusababisha maafa makubwa kwa watoto sehemu mbali mbali za dunia.

Kauli mbiu ya Maadhimisho ya Mwaka huu inajikita zaidi katika usawa katika Jamii, jambo ambalo linapaswa kuvaliwa njuga na wadau mbali mbali, ili kuboresha ushiriki wa wanawake katika mchakato wa maendeleo endelevu. Wanawake wanaojishughulisha na kilimo wawezeshwe kuzalisha mazao ya chakula na biashara, ili kuwa na uhakika wa chakula pamoja na kujijengea uwezo wa kiuchumi. Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa, FAO linasema kwamba, ikiwa kama wanawake watawezeshwa kikamilifu katika uzalishaji wanaweza kusaidia kupunguza kiasi cha watu millioni mia moja wanaoteseka kutokana na baa la njaa duniani.

Wanawake wamepewe haki ya kumiliki ardhi, wapate mikopo na pembejeo za kilimo, tayari kushiriki kikamilifu katika mchakato wa uzalishaji katika sekta ya kilimo. Wanawake wakiwezeshwa katika elimu na kilimo, baa la njaa na utapiamlo vitapewa kisogo duniani. Siku ya Wanawake Duniani ilianza kuadhimishwa mwaka 1975 na Umoja wa Mataifa.







All the contents on this site are copyrighted ©.