2014-03-07 11:13:22

Sierra Leone sasa ina amani na utulivu!


Kikosi cha kulinda amani cha Umoja wa Mataifa kilichokuwepo nchini Sierra Leone, kwa kipindi cha miaka kumi na mitano, kimehitimisha kazi yake na kufunga vilago, dalili kwamba, amani na utulivu vimerejea tena nchini humo. Vita iliyotokea nchini Sierra Leone kati ya Mwaka 1991 hadi kufikia mwaka 2002 vilisababisha vifo vya watu 50, 000 na nusu ya wananchi wa Sierra Leone walilazimika kuyakimbia makazi yao.

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Ban Kimoon akizungumza na waandishi wa habari mjini Freetown amekiri kwamba, Sierra Leone ni kati ya nchi ambazo zimefanikiwa kurejesha amani na utulivu na kwamba, kwa sasa Jeshi la kulinda amani la Umoja wa Mataifa linaweza kuondoka na kuwaacha wananchi wakiwa katika hali ya amani na usalama.

Changamoto kubwa iliyoko mbele ya Sierra Leone ni kuhakikisha kwamba, inatumia vyema rasilimali yake kwa ajili ya mchakato wa mapambano dhidi ya baa la ujinga, umaskini na maradhi yanayoendelea bado kusababisha majanga makubwa kwa wananchi wengi wa Sierra Leone.

Biashara na matumizi haramu ya dawa za kulevya, rushwa na makundi ya uhalifu ni kati ya mambo ambayo yanapaswa kufanyiwa kazi na Serikali ya Sierra Leone, ili kweli amani na utulivu vilivyopatikana kwa kumwaga damu ya wananchi wasiokuwa na hatia iweze kudumu na kuwa ni kikolezo cha ustawi na maendeleo ya wananchi wa Sierra Leone.







All the contents on this site are copyrighted ©.