Tume ya Haki na Amani ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania: TAMKO
Tamko “matumaini na furaha ya watanzania kwa ujio wa Rasimu ya katiba iliyosheheni
utu na misingi ya kujali maslahi ya wote”
Mkutano wa kitaifa wa wajumbe wa
kamati za majimbo za Haki na Amani za Kanisa Katoliki Tanzania pamoja na Wanataaluma
Wakristo wa Tanzania (CPT), walikutana kwenye Kituo cha kiroho cha Mbagala, Jijini
Dar es Salaam, tarehe 5 – 6 Februari, 2014.
Wakitafakari juu ya mchakato wa
kuandika Katiba Mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na wajibu wa Kanisa Katoliki
katika Utume wake wa Kinabii wa kulinda na kujenga haki na amani nchini mwetu, walimshukuru
Mungu kwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, chini ya uwenyekiti wa Jaji Joseph Sinde Warioba,
kufanikiwa kuwasilisha rasmi Rasimu Na. 2 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
kwa Rais Jakaya Mrisho Kikwete tarehe 30 Desemba, 2013 na kuashiria mwanzo wa hatua
ifuatayo ya kuunda Bunge Maalumu la Katiba.
Baada ya kuipitia Rasimu hiyo kwa
kuongozwa na uchambuzi makini uliowasilishwa na Sekretarieti ya Tume ya Haki na Amani
wajumbe wameridhia kwamba :
Kwa hakika Rasimu iliyowasilishwa
na Tume ya Mabadiliko ya Katiba ni ya watu na sio ya wanasiasa au vyama vya siasa
wala asasi za kidini. Kwa sababu hiyo tunatoa mwaliko kwa kila raia wa Tanzania kufurahia
ushiriki wake kufikia Rasimu Na. 2 yenye mambo bora yatakayokuwa nguzo ya umoja wa
nchi yetu katika Katiba Mpya.
Maadili yaliyomo
katika Rasimu Na. 2 ni muhimu kabisa kwa taifa letu. Wananchi na viongozi wote
sharti wajali maslahi kwa wote na wasimamie haki na wajibu wa kila mtu.
Madhumuni ya msingi ya Katiba ni ustawi wa kila Mtanzania, haki
za kiuchumi, usalama, kusikilizwa kabla ya kuhukumiwa na haki kwa wote pasipo ubaguzi
kwa madhumuni ya kulinda amani.
Katiba yetu
lazima isiruhusu wachache wenye nguvu za kisiasa, kiuchumi na kiutawala kutumia vibaya
uwezo wao na kusababisha utengano kitabaka katika jamii huku wakijinufaisha kwa kutumia
rasilimali za nchi zilizo za wote. Pawepo na udhibiti thabiti wa mienendo ya namna
hiyo na uwajibishaji makini kwa wabadhilifu wa mali ya umma.
Katiba ni chombo hai kwa ajili ya kuhudumia jamii na sio jamii kuhudumia
Katiba. Kwa sababu hiyo yatupasa kuthubutu kubuni njia mbadala ili kukuza kipato cha
raia wa kawaida na kuboresha huduma za jamii kwa kuwa na mipango endelevu ya kiuchumi.
Pendekezo la Muundo wa Muungano wa serikali
tatu sio jambo kuu kuliko mengine yote katika Rasimu hii. Muundo wa serikali mbili
haukutatua matatizo msingi bali ulilimbikiza kero zilizosababisha Zanzibar kujiundia
katiba yake mpya ya mwaka 2010 bila kushauriana na Tanzania Bara (Tanganyika). Pendekezo
la serikali tatu lililowekewa mazingira tekelezi yakitoa mwanya wa kuboresha muundo
huo kwa njia wazi, shirikishi na za kidemokrasi lina tija kubwa ya kuturudishia hali
ya kuwa wamoja.
Mihimili mikuu mitatu; Serikali
ya Jamhuri ya Muungano, Bunge la Jamhuri ya Muungano na Mahakama ya Jamhuri ya Muungano
ni taasisi mpya kabisa kwa mujibu wa Rasimu Na. 2 zitakazoongoza, kuratibu na kuwajibisha
kila kiungo cha Jamhuri ya Muungano zikiwemo serikali za Nchi Washirika.
Haki ya mtu ya kuishi lazima ilindwe na Katiba kuanzia pale mimba
ya binadamu inapo tungwa katika mama na katika hatua zake zote za kumhudumia mama
mjamzito.
Kumtambua Mungu na kumtaja katika
Katiba yetu kunamaanisha kukiri kwetu Uwepo Wake aliye Muumba wetu na vitu vyote ambavyo
mwanadamu anavitegemea kwa uhai wake. Mungu anakuwa rejelea yetu katika kuheshimiana
kiutu. Ni chimbuko la utu wa binadamu. Kwa kuwa katika Wimbo wetu wa Taifa tunamwomba
Mungu baraka zake ili tufanikiwe na tuishi kwa amani, ni hekima na busara kumkiri
katika Sheria Mama – Katiba.
Tunapoelekea kwenye Bunge Maalum la
Katiba tunataka mambo yafuatayo ya msingi kabisa yatambuliwe na kufahamika kwa wote:
Watanganyika na Wazanzibar tuwe na nia madhubuti ya kuwa wamoja.
Haki za binadamu za kisiasa, kiuchumi na kijamii zipatikane na
kufurahiwa na wote. Umasikini na ufinyu wa bajeti ya serikali ni visingizio tu vya
mamlaka kutokutoa haki kwa wote.
Yatupasa kukiri
mapungufu yetu katika serikali zetu na itikadi za kisiasa kusudi kwa moyo wa unyenyekevu
na mkunjufu tuanze safari mpya katika mwanga mpya wa maridhiano. Pamoja na kukiri
kasoro za wakati uliopita tujivunie maendeleo tuliyofanya katika kila nyanja za maisha
wakati tukiboresha mifumo na miundo ya utawala.
Ulimwenguni
hakuna katiba yoyote kamilifu. Yatupasa tuanze na Rasimu iliyopendekezwa na tuendelee
kuiboresha pale itakapobidi.
Tunawasihi wajumbe
wa Bunge Maalum la Katiba kuweka kando itikadi za vyama vyao kama walivyofanya Wanatume
wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba katika kuandaa Rasimu Na. 2. Bunge Maalum la Katiba
lilenge kufanikisha mchakato mwema wa Katiba Mpya itakayoandaa njia na mifumo mipya
ambayo kwayo tutahakikishiwa kuwepo kwa taratibu wajibishi na wajibikaji ili kuendeleza
ustawi wa jamii na muundo wa Muungano utakaokuwa wazi na tayari wakati wote kuboreshwa
kwa manufaa ya Watanzania wote.
Katiba Mpya
ya Tanzania itakuwa na fursa ya “FURAHA MPYA SHIRIKISHI” kwa Watanzania wengi. Rasimu
na. 2 ni hatua njema katika tukio muhimu la kihistoria nchini tanzania. Tunatarajia
bunge maalum lisimkane Mungu na lisikashifu mapendekezo ya serikali tatu.
Tunawaalika
wananchi wote wa Tanzania kwa dhamira moja, kuliombea na kulisaidia Bunge Maalum la
Katiba, liweze kufanya kazi yake kwa ustadi na kujali maslahi ya Taifa na wananchi
wote wa Tanzania.
Askofu Mkuu Paulo Ruzoka MWENYEKITI Tume ya
Haki na Amani - TEC