Kwaresima ni kipindi cha kujinyima kwa ajili ya jirani!
Katika mwenendo wa maadhimisho ya Mwaka wa Liturujia, Mama Kanisa ameweka kipindi
rasmi kwa ajili ya watoto wake kufanya toba na wongofu wa ndani; kufunga na kusali,
ili kujipatanisha na Mungu pamoja na jirani. Kusoma, kutafakari na kumwilisha Neno
la Mungu katika matendo ya huruma.
Hiki ni kipindi cha maandalizi ya kina
kabla ya maadhimisho ya Fumbo la Pasaka, yaani, mateso, kifo na ufufuko wa Yesu. Kwa
njia hii waamini wanashirikishwa upya uzima wa kimungu. Kanisa linawaandaa watoto
wake kwa Jumatano ya Majivu, kama mwanzo wa kipindi cha Kwaresima; mwaliko wa kutubu
na kufanya malipizi.
Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa watumiaji
wa mitandao ya kijamii anasema, Kwaresima ni kipindi muafaka cha kujinyima. Anawaalika
waamini na watu wote wenye mapenzi mema kujitahidi kujinyima kila siku kwa ajili ya
kufanya matendo ya huruma kwa jirani.