2014-03-04 08:59:42

Balozi wa Vatican aanza utume wake nchini Pwani ya Pembe


Hivi karibuni Askofu mkuu Joseph Spiteri, Balozi Mpya wa Vatican nchini Pwani ya Pembe aliwasili nchini humo na kupokelewa na viongozi wa Kanisa na Serikali kwenye Uwanja wa ndege wa Kimataifa mjini Abijan. Askofu mkuu Spiter baadaye alikutana na kuzungumza na Bwana Charles Koffi Diby, Waziri wa mambo ya nchi za nje, nchini Pwani ya Pembe, ambaye alimpatia nakala ya hati zake za utambulisho.

Tarehe 18 Desemba 2013, Askofu mkuu Joseph Spiter aliwasilisha hati zake za utambulisho kwa Rais Alassane Ouattara katika hafla ya kitaifa iliyokuwa imeandaliwa kwa heshima yake. Viongozi hawa wawili katika mazungumzo yao, wameridhika na uhusiano mwema uliopo kati ya Vatican na Pwani ya Pembe; kati ya Kanisa na Serikali katika mchakato wa haki, amani na upatanisho bila kusahau mchango mkubwa unaotolewa na Kanisa Katoliki katika sekta ya elimu, afya na maendeleo ya mtu mzima: kiroho na kimwili.

Kanisa linaendelea kujipambanua katika huduma zake kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Rais Alassane Ouattara amekumbusha kwa shukrani ziara ya kiserikali aliyoifanya mjini Vatican kunako 16 Novemba 2012 kwa kukutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI.

Askofu mkuu Joseph Spiteri amewasilisha salam na matashi mema kutoka kwa Baba Mtakatifu Francisko na kwamba, anapenda kutekeleza utume wake miongoni mwa Familia ya Mungu nchini Pwani ya Pembe kama mhudumu wa Injili anayependa kujenga na kudumisha udugu na mshikamano kati ya watu, ili kujenga na kudumisha utamaduni wa amani, kama anavyokazia Baba Mtakatifu Francisko.

Ilikuwa ni tarehe 14 Januari 2014, Askofu mkuu Joseph Spiteri alipowasilisha hati zake za utambulisho kwa Askofu Touabli Youlo, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Pwani ya Pembe kwa kutiwa mkwaju na aliyekuwa Askofu mkuu Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican ambaye hivi karibuni alisimikwa kuwa Kardinali. hafla hii imefanyika katika Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu, wakati ambapo Baraza la Maaskofu Pwani ya Pembe lilikuwa linaadhimisha mkutano wake wa 97.







All the contents on this site are copyrighted ©.