2014-03-04 10:14:21

Bado kuna watoto 50, 000 wanakabiliwa na utapiamlo na ukosefu wa huduma za afya nchini Somalia


Baa la njaa lililoikumba Somalia kunako mwaka 2011 linaanza kutoweka na kuna maendeleo pia katika masuala ya kisiasa ingawa bado kuna vitisho vya mashambulizi ya kigaidi. Licha ya Somalia kuanza kuonesha cheche za maendeleo, lakini Umoja wa Mataifa pamoja na Serikali ya Somalia inawahimiza wafadhili mbali mbali kuendelea kuchangia katika ustawi na maendeleo ya Somalia. Kuna zaidi ya watoto 50, 000 wanaokabiliwa na utapiamlo wa kutisha pamoja ukosefu wa huduma msingi za afya.

Jumuiya ya Kimataifa kwa sasa inaelekeza misaada yake Sudan ya Kusini, Syria na Jamhuri ya Watu wa Afrika ya Kati ambako watu kwa sasa wanakabiliana na maafa makubwa. Lakini Serikali ya Somalia inasema, bado wanahitaji msaada kutoka kwa Jumuiya ya Kimataifa ili kuokoa maisha ya watoto wanaokabiliwa na utapiamlo wa kutisha pamoja na ukosefu wa huduma msingi za afya.

Rushwa na ubadhirifu wa mali ya umma pamoja na misaada inayotolewa kwa wananchi wa Somalia ni kati ya mambo yanayokwamisha utoaji wa misaada inayopelekwa nchini Somalia, kadiri ya taarifa ya Umoja wa Mataifa. Bado asilimia 60% ya watu wapatao millioni 3.5 wako chini ya utawala wa Kikundi cha Kigaidi cha Al Shabab, Kusini mwa Somalia. Umoja wa Mataifa unaohifia kwamba, ikiwa kama wananchi watashambuliwa wakati huu wa kutayarisha mashamba, mavuno hapo mwakani yanaweza kuwa ni hafifu.







All the contents on this site are copyrighted ©.