2014-03-03 08:53:33

Kipindi cha Kwaresima ndani ya Familia


Mpendwa msikilizaji wa Radio Vatican, kwa mara nyingine karibu katika Kipindi chetu cha Kanisa la nyumbani, ambapo leo, tunaandaana kuanza safari yetu ndefu na muhimu sana ya mfungo wa siku arobaini (mfungo wa Kwaresma), tutakayoianza siku ya Jumatano ya majivu. RealAudioMP3
Katika kipindi hiki cha siku 40, mama Kanisa anatualika sisi sote kushughulikia kwa jitihada kubwa zaidi uongofu wetu sisi wenyewe. Masomo matakatifu pamoja na tafakari nyingi, zitatuelekeza kujitafiti katika roho ya ukweli wa ndani, tujifahamu tulivyo ili tujirekebishe pale ambapo hatukwenda sana na tujiimarishe zaidi pale ambapo kwa neema ya Mungu tuliweza kwenda sawa. Daima sote tunaalikwa kuongeza na kuimarisha maisha ya fadhila mbalimbali.
Kwaresma ni kipindi cha kujipatanisha kwanza na nafsi zetu. Kuna nyakati tumejitendea mambo makubwa maovu sana, hata tukaanza kujichukia sisi wenyewe, tumejikatia matumaini, tunajiona hatufai tena na tunahisi kuwa hatupendwi na wenzetu. Hatua ya kwanza ya wongofu ni kujifahamu, pili ni kujikubali na tatu ni kuwa tayari kujisamehe na kujirekebisha. Acha ya kale, anza upya, songa mbele.
Kwaresma ni kipindi cha kumrudia Mungu kwa mioyo yetu yote. Kwa kinywa cha Nabii Yoeli mwenyewe asema “...nirudieni mimi kwa moyo wote, kwa kufunga, kulia na kuomboleza” Yoel 2:12. Katika roho ya ukweli wa ndani, kila mmoja katika familia anajua ni namna gani amejiweka mbali na Mungu, na kwa kitendo cha kuwa mbali na Mungu, wewe katika familia umekuwa ndio uchochoro wa shetani, anayeingia katika familia ili kuivuruga. Bwana akuita kwa upole, asema nirudieni mimi kwa moyo wote.
Kwaresma ni kipindi cha kutoa sadaka sana, kusali sana kwa moyo wa toba ya ndani na kufunga (Rej. Mt. 6:1-6, 16-18). Hii ni sehemu ya habari njema inayosomwa siku ya Jumatano ya Majivu. Katika sehemu hii Bwana anatupatia nidhamu ya kutoa sadaka, kusali na kufunga ili kweli tupate mafaa ya kiroho. Na sisi kama familia tunapenda kwaresma hii tuwe na sadaka ya pamoja kama familia, tuwe na sala za pamoja zaidi na tuuchukue mfungo huu kwa pamoja. Wataalamu wa mambo ya roho wanatuambia, kufunga ni namna bora zaidi ya kufanya kitubio na kujipatia nguvu mpya ya roho.
Kwa ujumla wake katika kipindi hiki cha Kwaresma, sisi wana kanisa la nyumbani yaani familia, tutatafakari sana juu ya tunu za toba na msamaha. Tutakiri kwamba, katika familia zetu mara nyingi tumekoseana na kujeruhiana vibaya sana, kiasi kwamba tumeathiri vikali ule UZURI wa maisha ya ndoa na familia. Kwa matendo yetu tumeifukuza haki, tumefukuza upendo, tumefukuza amani na furaha ya familia. Dawa yetu ni mmoja tu – toba na msamaha, tufanye toba ya kweli, tusameheane na tuwe tayari kujirekebisha kabisa.
Familia nyingi zimekonda na kunyauka vibaya, hazijui tena kicheko wala tabasamu, wala utani kwa sababu wanashindwa kuombana msamaha wa kweli na kusameheana. Wengi wanapenda zaidi maisha ya ubabe na umame ambayo hayajengi familia kamwe. Ugangwe, jeuri, kiburi na roho mbaya vinaelekea kutawala katika familia zetu!! Vilio vimezidi katika Kanisa la nyumbani. Nani anyamazishe? Ni MIMI NA WEWE.
Baba Mtakatifu Fransisko anatufundisha, maneno matatu yanayoifanya familia isonge mbele ni NAOMBA, SAMAHANI na ASANTE. Katika Kwaresma hii tutalitafakari sana hilo lihusulo KUOMBA MSAMAHA, KUTUBU KWA MANENO NA VITENDO, na KUFANYA JITIHADA YA KUJIREKEBISHA. Usijitese kwa kutokuwa tayari kutubu, na usijiangamize kwa kutokuwa tayari kusamehe.
Mume jipatanishe na mkeo, mke jipatanishe na mumeo, wazazi jipatanisheni na watoto wenu, watoto, jipatanisheni na wazazi wenu. Msamaha na mapatano mema VINAWEZEKANA. Bwana Mungu atuumbie mioyo safi na atengeneze tena roho thabiti iliyotulia ndani mwetu. Tunawaweka mikononi mwa Mungu na tunawatakieni nyote Kwaresma njema. Kutoka katika Studio za Radio Vatican ni mimi Padre Pambo Martin Mkorwe OSB.








All the contents on this site are copyrighted ©.