2014-03-01 16:05:41

Waziri mkuu Ponta wa Romania akutana na Papa Francisko mjini Varican


Baba Mtakatifu Francisko, Jumamosi tarehe 1 Machi 2014 amekutana na kuzungumza na Waziri mkuu Victor Ponta wa Romania, ambaye baadaye alikutana na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican aliyekuwa ameambatana na Askofu mkuu Dominique Mamberti, Katibu mkuu wa mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican.

Waziri mkuu Ponta amewasilisha salam na matashi mema kutoka kwa Patriaki Daniele wa Kanisa la Kiorthodox. Kiini cha mazungumzo kati ya Baba Mtakatifu Francisko na mgeni wake kilikuwa ni familia, elimu, uhuru wa kidini na umuhimu wa kusimama kidete kulinda na kutetea tunu msingi za maisha ya kiutu na kiroho zinazojipambanua katika ushirikiano kati ya Vatican na Romania mintarafu Jumuiya ya Kimataifa.

Viongozi hawa wamepongeza mchango mkubwa unaotolewa na Kanisa Katoliki nchini Romania kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wananchi wa Romania. Wamegusia pia mambo yanayopewa kipaumbele cha kwanza na Kanisa Katoliki nchini humo. Mwishoni, viongozi hawa wawili wamebadilishana mawazo kuhusu hali ya kimataifa kwa kukazia umuhimu wa majadiliano ya kina ili kukomesha vita na kinzani za kijamii zinazoendelea kujitokeza sehemu mbali mbali za dunia.







All the contents on this site are copyrighted ©.