2014-03-01 10:29:59

Onesheni imani katika matendo kwa kuchangia Nchi Takatifu


Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makanisa ya Mashariki limepokea changamoto na wasi wasi uliooneshwa Baba Mtakatifu Francisko kwa ajili ya Makanisa ya Mashariki, linawaalika waamini wa Makanisa mahalia sehemu mbali mbali za dunia, kuonesha mshikamano wao wa dhati kwa Wakristo wa Makanisa ya Mashariki, wakati wa kipindi cha Kwaresima kwa kuchangia kwa hali na mali, ustawi na maendeleo ya watu hawa kiroho na kimwili.

Waamini na watu wote wenye mapenzi mema wanakumbushwa kwamba, Baba Mtakatifu Francisko kwa Mwaka huu anapenda kuyaelekeza macho yake zaidi huko Syria, Iraq, Misri na Nchi Takatifu, ili kuhakikisha kwamba, amani na utulivu vinapatikana; watu wanaheshimiwa na kuthaminiwa utu wao kama binadamu pamoja na kupata mahitaji yao msingi. Waamini wanaweza kuonesha mshikamano wao kwa kuchangia ustawi na maendeleo ya watu wanaoishi huko Mashariki ya Kati.

Kardinali Leonardi Sandri, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa kwa ajili ya Makanisa ya Mashariki katika barua yake kwa Maaskofu mahalia anawakumbusha kwamba, sadaka itakayokusanywa Ijumaa kuu kwa Mwaka 2014 itakuwa ni kwa ajili ya kusaidia na kuenzi shughuli mbali mbali za kichungaji zinazotekelezwa na Jumuiya za Waamini katika Nchi Takatifu. Msaada wao wa hali na mali usindikizwe pia kwa njia ya sala.

Ukarabati wa Kanisa la Kuzaliwa Bwana mjini Bethlehemu ni kati ya miradi iliyofanyiwa kazi kutokana na sadaka iliyokusanywa Ijumaa kuu katika Mwaka 2013. Ukarabati huu pia umechangiwa kwa kiasi kikubwa na juhudi za kiekumene. Mchango wa Kanisa Katoliki katika sekta ya elimu bado unahitajika sana anasema Kardinali Sandri. Tatizo la wakimbizi, wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi ni mambo ambayo pia yanachangiwa na fedha zinazokusanywa kutoka Majimboni. Watu hawa wengi wao wanaendelea kuhudumiwa na Jumuiya za Kikristo huko Mashariki ya Kati.

Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake wa Kwaresima anamwomba Roho Mtakatifu ili aweze kuwasaidia waamini kutekeleza wajibu wao kwa kuajibika kikamilifu kwa kuonesha mshikamano wa dhati na wale wote wanaoteseka kutokana na sababu mbali mbali, ili kuwa kweli ni watu wenye huruma inayomwilishwa kwenye matendo ya huruma kwa maskini na wahitaji zaidi.

Nchi Takatifu ina kiu ya msaada huu unaoneshwa na waamini kutoka kwenye Makanisa mahalia, kama kielelezo makini cha imani tendaji. Mshikamano wa upendo ni kielelezo makini cha maandalizi ya Hija ya Kichungaji itakayofanywa na Baba Mtakatifu Nchi Takatifu, hii ni hija ya furaha na matumaini kwa Watu wa Mungu wanaoishi katika Nchi Takatifu.







All the contents on this site are copyrighted ©.