Kwaresima ni kipindi cha toba na wongofu wa ndani!
Tazama, wakati uliokubalika ndio sasa; tazama, siku ya wokovu ndiyo sasa. Hii ndiyo
kauli mbiu inayoongoza ujumbe wa Kwaresima kwa Mwaka 2014 kutoka kwa Patriaki Bartolomeo
wa kwanza wa Kanisa la Kiorthodox la Costantinopoli anayewaalika waamini kutubu na
kumwongokea Mwenyezi Mungu.
Toba ni kati ya mafundisho ya kwanza yaliyotolewa
na Yesu mwenyewe na huu ni mwaliko endelevu unaotolewa na Mama Kanisa kwa watoto wake.
Pamoja na mwaliko wote huu, lakini bado Wakristo wengi hawajaweza kumwilisha ujumbe
huu katika uhalisia na undani wa maisha yao; ujumbe unaogusa dhamiri, kwani dhana
ya dhambi inaonekana kutoweka kwa wengi.
Wongofu unawawajibisha hata watakakatifu
ili wasirudie tena nafasi za dhambi na hatimaye kutenda dhambi, tayari kubadilika
na kuchuchumilia mambo makubwa na dumifu katika ujenzi wa mahusiano mema na Mwenyezi
Mungu pamoja na ulimwengu. Lengo ni kukoleza fadhila ya upendo, unyenyekevu, toba
na amani.
Patriaki Bartolomeo wa kwanza anasema, wongofu wa ndani ni hija
isiyokuwa na mwisho inayopania kushiriki utakatifu wa maisha ya Kimungu. Ili kufikia
lengo hili kuna haja kwa waamini kuwa na mikakati ya maisha ya kiroho inayowawajibisha
kubadilika kama anavyosema Mtakatifu Paulo anapowaandikia Wakorintho "Lakini sisi
sote, kwa uso usiotiwa utaji, tukiurudisha utukufu wa Bwana, kama vile katika kioo,
tunabadilishwa tufanane na mfao huo huo toka utukufu hata utukufu, kama vile kwa utukufu
utokao kwa Bwana, aliye Roho."
Utakaso wa ndani unapania kusafisha jicho la
maisha ya kiroho na hivyo kumwezesha mwamini kujiona kutoka katika undani wake, ili
kuwa na roho mpya ya mwana mpendwa wa Mungu, aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.
Wongofu wa ndani unapaswa kuzaa matunda ya msamaha na mtendo ya huruma kwa jirani;
kwa kumpokea na kumwonjesha ukarimu kadiri inavyowezekana pamoja na kumsaidia kupata
mahitaji yake msingi. Hiki ni kielelezo cha msingi wa toba ya kweli.
Sehemu
ya pili ya utakaso ni kwa waamini kutubu, kuungama dhambi na kujikita katika maisha
ya sala katika upendo, unyenyekevu, kwa kushinda ubaya kwa wema; kwa kukimbia nafasi
za dhambi na bila kukumbatiwa na malimwengu kwani haya ni chanzo cha kifo cha maisha
ya kiroho. Waamini washinde kishawishi cha kiburi na unafiki wa kifarisayo kwa kutambua
kwamba, wote ni wadhambi na wanahitaji kuonjeshwa upendo na huruma ya Mungu.
Kipindi
cha Kwaresima kinakuja wakati bado kuna watu wanaendelea kukabiliana na athari za
myumbo wa uchumi kimataifa; watu ambao wanapaswa kuonja huruma na mshikamano wa upendo
kama kielelezo cha mabadiliko ya ndani na matunda ya toba na wongofu wa kweli. Iwe
ni nafasi ya kujinausa kutoka katika dhambi na ubinafsi, kwa kujishikamanisha na Mwenyezi
Mungu kwa njia ya fadhila ya unyenyekevu, ili kuomba huruma ya Mungu kama alivyofanya
yule Mtoza ushuru aliyehesabiwa haki pale Hekaluni.
Kwaresima kiwe ni kipindi
cha toba na wongofu wa ndani kama sehemu ya mchakato wa maandalizi ya kushiriki mateso,
kifo na ufufuko wa Kristo, si tu kwa njia ya maneno matupu ambayo kamwe "hayawezi
kuvunja mfupa" bali kwa njia ya imani tendaji inayoshuhudiwa katika uhalisia wa maisha.
Ni kipindi cha kujishughulisha na maisha mapya yanayofumbatwa katika neema.
Patriaki
Bartolomeo wa kwanza anasema, ni fursa kwa waamini kutambua umuhimu wa kutubu, kuongoka
na kuchuchumilia wokovu kwa kufanya wongofu wa kweli, kutokana na uwepo wa dhambi
walizotenda. Anawatakia kheri na baraka tele katika Kipindi cha Kwaresima.