2014-03-01 08:24:02

Endelezeni huduma ya huruma na upendo wa Mungu kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii


Baba Mtakatifu Francisko anawaalika kwa namna ya pekee wajumbe wa Chama cha Kitume cha Mtakatifu Petro kuendelea kuonesha upendo wa Mungu na Kristo kwa njia ya matendo ya huruma yanayofanywa kwa ajili ya maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii na mahujaji wanaomiminika kila siku mjini Roma kwa niaba ya Kanisa.

Ujumbe wa Baba Mtakatifu Francisko umesomwa kwa niaba yake na Askofu mkuu Georg Ganswen, Mkuu wa Nyumba ya Kipapa, wakati wa maadhimisho ya kumbu kumbu ya miaka 145 tangu chama hiki kilipoanzishwa. Mkutano huu umefanyika tarehe 27 Februari 2014. Wajumbe wamehimizwa kuendeleza matendo ya huruma kwa niaba ya Baba Mtakatifu si tu kwa maskini na wale wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, bali huduma hii pia iwafikie wagonjwa na familia zinazokabiliana na hali ngumu ya maisha kutokana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa.

Wajumbe wametakiwa kujielekeza katika kusaidia katekesi endelevu na kwa vijana wanaojiandaa kwa ajili ya kupokea Ekaristi Takatifu, vituo vya Katekesi hata kwenye vituo vya mazoezi ya vungo. Yote haya ni makundi yanayohitaji kuonja huruma na upendo wa Mama Kanisa kwa njia ya huduma za maisha ya kiroho na kimwili.Wajumbe waonje na kuguswa na mahangaiko ya watu katika medani mbali mbali za maisha.

Rais Giorgio Napolitano wa Italia kwa kutambua mchango wa Chama cha Kitume cha Mtakatifu Petro, ametuma ujumbe na matashi mema kwa wajumbe wa mkutano huu, uliowashirikisha viongozi wakuu wa Kanisa na Serikali ya Italia; wanajeshi na wadau mbali mbali wa masuala ya mshikamano na utengamano wa kijamii.

Mwishoni wa mkutano huu, wajumbe wapya walipata nafasi ya kula kiapo pamoja na kuwatunuku nishani wanachama ambao wamedumu katika Chama hiki kwa kipindi cha miaka ishirini na mitano, kwa kutambua mchango wao katika kukuza na kuendeleza utamaduni wa mshikamano na upendo kati ya watu.







All the contents on this site are copyrighted ©.