Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya VIII ya Kipindi cha Mwaka A wa Kanisa
Mpendwa msikilizaji wa kipindi tafakari masomo Dominika, niko pamoja nawe tena katika
Dominika hii ya VIII ya mwaka A wa Kanisa kukushirikisha furaha yangu toka meza ya
Neno la Mungu.
Mwaliko toka
Neno lenyewe ni kwamba kamwe Mungu hawezi kuwasahau watoto wake. Ndiyo kusema kiitikio
cha wimbo wa mwanzo kioneshacho tumaini la mzaburi yakwamba Bwana ndiye tegemeo lake
daima kinatupa kielelezo murua juu ya upendo wa Mungu kwa watu wake.
Somo la
kwanza tunalipata toka Kitabu cha Nabii Isaya ambamo tunamwona Nabii akiwambia Waisraeli
watulie na waw na matumaini katika mateso yao. Wanaalikwa kutambua kuwa, pamoja na
kwamba wako utumwani Babeli, Mungu ni mkuu na kamwe hataweza kuwaacha katika taabu
hiyo. Anawaambia waachane na mantiki ya kuuona utendaji wa Mungu kama utendaji wa
mwanadamu ambaye huweza kuwasahau watoto wake. Tunakumbuka katika Israeli kama mmoja
aliachana na mke wake haikuwa rahisi tena kurudiana naye, na ilikuwa pia hivyohivyo
kama mzazi alimfukuza mtoto wake haikuwa tena ruhusa kumrudisha nyumbani. Ni mambo
ya ajabu haya lakini ndo hali ya mwanadamu.
Mpendwa mwana wa Mungu, ni katika
mantiki hiyohiyo Waisraeli walipoenda utumwani Babeli kwa sababu ya dhambi na ukaidi
wao, walijiona ni kama mwanamke au mtoto aliyefukuzwa nyumbani na hawezi kurudi tena
nyumbani. Basi Nabii akitumwa na Mungu anawatuliza akiwakemea kwa sababu ya mawazo
yao hayo potofu. Anaweka mbele yao maneno ya Mungu akisema hivi mama aweza kumsahau
mwanae anayenyonya? Na hata akimsahau, Mimi Mungu wenu sitaweza kuwasahau ninyi. Mungu
anahakikisha ukuu wake na upendo usiopimika kwa maana ya vipimo vya kifalsafa. Mpendwa
tukumbuke! “akamtuma Mwanaye wa pekee, akatwaa mwili wetu kwa ajili ya wokovu wetu!!
Katika
somo la pili Mt. Paulo anawaandikia Wakorinto akiwaonya na kuwaambia kuwa kuhubiri
kwake hakutegemei hekima yake kama binadamu bali hekima ya kimungu. Kumbe anawaomba
waelewe kwamba yeye pamoja na wahubiri wengine ni watumishi na wagawaji wa mafumbo
ya Mungu. Wakorinto walikuwa na mashaka juu ya mahubiri ya Paulo na hivi kuonesha
ukaidi fulani kitu ambacho hivi leo kinazidi kutunyemelea hata sisi watangazaji wa
Neno la Mungu. Ukaidi wa Wakorinto ulilala katika mantiki ya kuweka mawazo yao katika
wale waliokwishatangulia kuhubiri imani ya Kikristu kwao.
Basi Mt Paulo anakemea
hilo na kusema hivi wahubiri ni akina nani? Paulo anazidi kujiuliza hivi Wahubiri
wawezaje kuwa ndiyo chanzo cha mgawanyiko katika jumuiya? Ndiyo kusema anataka wahubiri
waeleweke kama watumishi wa Neno la Mungu na kwa jinsi hiyo basi, wahubiri si wa kutukuza
bali tunaalikwa kumtukuza Mungu. Mpendwa ni katika mantiki hii, kamwe hatutaweza kuwaweka
wahubiri mbele na badala yake lazima kumweka Mungu mbele aliye taa ya maisha yetu
na kisima cha hekima.
Mpendwa msikilizaji, wewe uliyemhubiri wa Neno la Mungu
unaalikwa kuweka neno moja kichwani mwako yaani lile la kupeleka ujumbe wa habari
njema kwa uaminifu bila kupunguza kitu wala kuongeza chochote kwa sifa na utukufu
wa Mungu. Mt. Paulo anatuangalisha kwa makini katika maisha ya kitume ili kuepuka
kuyumbishwa na mawazo potofu yatokayo kwa wale wapokeaji wa mafumbo ya Mungu na pia
kuyumbishwa na mawazo yetu sisi wenyewe.
Katika somo la Injili tunakutana na
mafundisho ya Bwana ambayo yakazia kuchagua kwa uthabiti kabisa kumtumikia Mungu au
kutumikia mali. Ndiyo kusema haitawezekana kumtumikia Mungu na wakati huohuo ukitumikia
miungu inayowakilishwa na mali au fedha. Bwana anasema yatupasa kuwa makini akitoa
mfano rahisi lakini ulio na uzito! Anasema hivi hata ukihangaika kwa ukitafuta mali
waweza kujiongezea kimo chako? Asema tena Je,? kama maua ya kondeni Mungu ayafanya
yapendeze hivi je kwetu sisi watoto wake wapendwa, hatafanya zaidi?, kwa nini tunajihangaisha?
Baada ya maswali haya, Bwana anasema “tafuteni kwanza ufalme wa mbingu mengine yote
mtayapewa kwa ziada”! Mpendwa msikilizaji, ndiyo kusema, Mungu hatatuacha wala kutusahau
bali yuko pamoja nasi.
Mpendwa msikilizaji, yafaa kujiuliza kidogo hivi hatari
ya fedha au mali yamnyemelea nani? Wa hakika hatari hii inawanyemelea matajiri na
maskini kwa ujumla wao. Kumbuka amri ya ya kwanza ya Mungu, inayoelekezwa kwa wote
maskini na tajiri ikisema, ndimi Bwana Mungu wako usiabudu miungu wengine. Kut. 20:3.
Kwa hivi mpendwa msikilizaji lazima kuwa makini tusije kuanguka katika falisafa ya
kuwatazama matajiri kama ndio wanaoguswa na jambo hili. Tukisonga mbele katika tafakari
tunajiuliza tena, hivi mali yawezaje kuwa muungu wakati ni kitu cha kugusika? Kwa
hakika mali hugeuka na kuwa muungu wakati tunapoweka mawazo yetu katika mali hiyohiyo!
Katika hili tunasaidiwa kuelewa tunapokumbuka wajibu wetu wa kumpenda Mungu
kwa akili na kwa mawazo yetu yote!! Mpendwa mwana wa Mungu yafaa kujiuliza hivi katika
Biblia miungu yatajwa kwa majina gani? Kwa hakika katika Biblia tunakutana na miungu
midogo kama vinywaji vinavyotupeleka katika ulevi, fedha, uasherati, tabia fulani
katika tamaduni zetu nk. Mwaliko kwetu ni kuwa makini kupambana na vinyemelezi hivi
katika maisha yetu.
Katika Injili ya Dominika hii kile kinchotajwa kama mungu
ni fedha. Tunajiuliza kwa nini fedha wakati fedha tunatambua ni kwa ajili ya mabadilishano?
Fedha inakuwa kiwakilishi cha miungu kwa sababu kama mtu aliyenazo si mwadilifu aweza
kujipatia kila aina ya kitu kinyume na hali ya kawaida. Mtu huyo aweza kufanya safari
haramu, aweza kununua kura haramu, aweza kula na kusaza na kutupa chakula, aweza kuwahonga
wasimamizi wa hifadhi za taifa na kupora tembo na mambo kama hayo. Ndiyo kusema polepole
ndani ya mtu hukua na kukomaa mawazo kinyume na utu wa kawaida.
Ni katika
kukomaa kwa mawazo haya mtu huweza kuacha hata mke wake au mme wake, huweza kuacha
watoto wake katika taabu, huweza kusahau masilahi ya taifa lake, huweza hata kuua
katika mantiki ya kujilinda na mambo kama hayo. Huu ndio muungu, ndio uondoaji wa
heshima na uhuru kwa mtu mwenye fedha na mawazo ya fedha na mali kwa ujumla.
Mpendwa
msikilizaji yafaa kujiuliza swali jingine, hivi ni kwa nini Mungu na fedha au mali
si rahisi kukaa pamoja? Kwa hakika fedha au mali anayo falisafa ya kuongeza mali na
fedha kwa namna yoyote. Matokeo ya hili ni kuwanyonya maskini na hata kuwatupilia
mbali. Ni kuwanyima dawa wanaougua, ni kuwapiga na kuwajeruhi wale wanaodai haki kwa
ajili ya masilahi ya taifa na jumuiya kwa ujumla. Kama ni wapangaji wake wa nyumba,
basi mali ataka walipe hata kwa udi na uvumba vinginevyo ni kuwatoa nje ya nyumba,
tena zaidi ongezeko la kodi bila utaratibu!
Wakati mali akisisitiza falisafa
ya ongezeko la mali, Mungu asisitiza na kurudia kinyume cha mali akisema mpende jirani
yako, heri walio maskini wa roho, heri wanaothamini masilahi ya taifa na watu, msaidie
mwenye shida na mfunge vidonda mwenye taabu kama alivyofanya Msamaria mwema na hapa
kuna maisha na tuzo ya uzima. Hizi falsafa mbili haziwezi kukaa pamoja, kumbe mwanadamu
lazima achague kuishi! yaani falisafa ya upendo kwa Mungu na kwa watu.
Sehemu
ya pili ya Injili inatukumbusha kuwa watu wa kujenga amani moyoni, yaani, kumtegemea
Mungu daima. Kumbuka wimbo wetu usemao “palipo na mapendo hapo Mungu yupo” maana yake
tujishughulishe na shughuli za upendo na Mungu atakuwa nasi daima. Mpendwa yafaa kuwa
makini sana tunapoisoma Injili hii, maana mwanzoni mwa sehemu ya pili inasema msijihangaishe
mtakula nini, angalieni maua ya kondeni na ndege wa angani.
Kumbe yaweza kupelekea
tukaacha kufanya kazi! Kwa hakika Bwana apenda tuwajibike, kumbe Injili haisemi msifanye
kazi bali inasema msiwe na wasiwasi, ndiyo kusema wakati mkifanya kazi mtegemee Mungu
na yote yataenda. Narudia kusema Mungu ataka tuwe na utulivu na amani moyoni mwetu
lilillo tunda la Roho Mtakatifu na si tuwe wavivu na wajanja wa mtaani!
Mpendwa
mwana wa Mungu, tunaalikwa kuwa na amani kwa sababu maisha yetu yako ndani ya moyo
wa Mungu. “yeye aliyeanzisha kazi yake ajua kuiendeleza”-Mtakatifu Gaspari. Ndiyo
kusema, unaalikwa kutambua kuwa kazi yoyote njema ukiikabidhi mikononi mwa Mungu itafaulu
daima. Aidha Mungu habezi mali bali akataa mali kuchukua nafasi ya Mungu. Ndiyo kusema
mali iwe kwa ajili ya kumtumikia yeye. Tumia na zalisha mali kwa kuwasaidia watu wa
Mungu: jenga shule, anzisha vituo vya yatima, saidia watu wanaohitaji msaada wa kisheria
na tumia mali kujenga ustawi wa familia yako na kukomaza mapendo kwa watu na Mungu. Mpendwa
ninakutakia furaha na matumaini katika maisha yako daima ukimtanguliza Mungu na kwa
namna hiyo kuijua hekima ya kweli itokayo kwa Mungu. Tumsifu Yesu Kristo. Tafakari
hii imeletwa kwako na Padre Richard Tiganya, C.PP.S.