2014-02-28 11:56:03

Papa Francisko achambua uzuri na utakatifu wa ndoa


Uzuri na utakatifu wa maisha ya Sakramenti ya Ndoa unaweza kueleweka vyema zaidi kwa kufanya rejea kwa Kristo na Kanisa lake. Wana ndoa katika shida na mahangaiko yao ya ndani wanapaswa kusaidiwa na wala si kuhukumiwa na kwamba, Yesu Kristo ndiye Mchumba mwaminifu wa Kanisa lake. Haya yamesemwa na Baba Mtakatifu Francisko wakati wa mahubiri yake kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Martha, kilichoko mjini Vatican, Ijumaa tarehe 28 Februari 2014.

Mafarisayo na Walimu wa Sheria walitaka kumpokonya Yesu mamlaka yake ya kimaadili kwa kumtega na swali kuhusu ndoa na talaka. Ni swali linaolenga kuvuruga uhusiano kati ya Mungu na binadamu na kati ya wanandoa, lakini Yesu anawakumbusha kwamba, tangu mwanzo Mwenyezi Mungu alimuumba mwanaume na mwanamke wanaounda familia na kuwa ni kitu kimoja. Muungano huu kati ya mwanaume na mwanamke unaonesha utukufu wa Mungu katika kazi ya Uumbaji.

Mwenyezi Mungu anampatia Adamu mwenza wa hija ya maisha; upendo unaoendelea kujionesha katika maisha ya mwanadamu, hata pale mwanadamu aliposhindwa kuwa mwaminifu, lakini bado Mwenyezi Mungu aliendelea kumwonjesha upendo usiokuwa na kifani! Upendo kati ya Kristo na Kanisa lake unafafanuliwa vyema na Mtakatifu Paulo katika Nyaraka zake. Huu ndio ule uhusiano kati ya Mungu na Waisraeli katika Agano la Kale; Kristo na Kanisa lake katika Agano Jipya.

Baba Mtakatifu anawaalika waamini na watu wenye mapenzi mema kusikia uchungu pale pendo linapovurugika na kuingia mchanga, mwaliko wa kuwasindikiza wale ambao pendo lao limemeguka badala ya kuwalaani na kuwakashfu. Hii ndiyo sheria ya upendo wa Kikristo kwa wanandoa kadiri ya Mpango wa Mungu unaowashirikisha katika kazi ya Uumbaji.

Huu ndio uzuri wa maisha ya ndoa na familia ya Kikristo, changamoto na mwaliko wa kuwaenzi wanandoa katika hija ya maisha yao ya ndoa na familia. Kwa wanandoa ambao upendo wao umemeguka wasaidiwe kuonja tena upendo wa Kristo na Kanisa lake. Wanandoa wajifunze kushinda kishawishi cha kutalakiana; watambue kwamba, ndoa ni upendo dumifu hadi kifo kitakapowatenganisha.







All the contents on this site are copyrighted ©.