2014-02-28 10:16:06

Papa akutana na viongozi wa kidini kutoka Argentina


Baba Mtakatifu Francisko, Alhamisi jioni tarehe 27 Februari 2014 amekutana na kuzungumza na Kikundi cha viongozi 45, kutoka dini ya Kiislam, Kiyahudi na Kikatoliki kutoka Argentina, waliokuwa wanarejea kutoka katika hija ya maisha ya kiroho katika Nchi Takatifu.

Viongozi hawa wametembelea katika maeneo ambayo Baba Mtakatifu Francisko katika hija yake ya kichungaji Nchi Takatifu ataifanya, yaani Yordani, Israeli na Palestina. Viongozi hawa wamekutana na kuzungumza na viongozi wa kidini na kisiasa katika maeneo haya.

Hiki ni kikundi cha viongozi wa kidini ambacho bado kinaendeleza ushirikiano na Baba Mtakatifu Francisko katika msingi wa maisha ya kiroho, ndiyo maana viongozi hawa wamehitimisha hija yao ya maisha ya kiroho kwa kukutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu Francisko.

Mkutano huu umehudhuriwa pia na viongozi wa Baraza la Kipapa la Uhamasishaji wa Umoja wa Wakristo pamoja na Baraza la Kipapa la Majadiliano ya Kidini. Hayo yamefafanuliwa na Padre Federico Lombardi, Msemaji mkuu wa Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.