2014-02-27 10:46:23

Majandokasisi wa Jimbo kuu la Roma wanasubiri kwa hamu kukutana na kuzungumza na Papa Francisko


Baba Mtakatifu Francisko katika Maadhimisho ya Kumbu kumbu ya Bikira Maria, Mama wa Imani, Msimamizi wa Jumuiya Seminari ya Jimbo kuu la Roma, Ijumaa jioni tarehe 28 Februari 2014 anatarajiwa kutembelea na kuzungumza na Waseminari wa Seminari kuu ya Jimbo kuu la Roma, kwenye Eneo la Chuo Kikuu cha Kipapa cha Laterano, kilichoko mjini Roma.

Huu utakuwa ni mwanzo wa Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka Mia Moja tangu Bikira Maria Mama wa Imani alipochaguliwa kuwa Msimamizi wa Jumuiya hii ya malezi kwa Jimbo kuu la Roma. Tarehe Mosi, Machi, 2014, Kardinali Agustino Vallini, Makamu Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Roma, anatarajiwa kuongoza Ibada ya Misa Takatifu majira ya asubuhi kama sehemu ya Maadhimisho haya.

Itakuwa ni mara ya kwanza kwa Baba Mtakatifu Francisko kukutana na kuzungumza na Jumuiya ya Malezi ya Jimbo kuu la Roma ambayo kwa sasa ina jumla ya Waseminari 80 pamoja na walezi wao. Mkutano huu wa Baba Mtakatifu utawajumuisha pia na Waseminari kutoka Seminari zilizoko mjini Roma pamoja na kujibu maswali yatakayoulizwa na Majandokasisi. Baba Mtakatifu Francisko atahitimisha mkutano huu kwa kupata chakula cha usiku pamoja na Jumuiya nzima ya Seminari kuu ya Jimbo kuu la Roma.







All the contents on this site are copyrighted ©.