2014-02-26 08:37:19

Hatari zinazowakabili Askari watoto!


Askari watoto wanaopelekwa mstari wa mbele kupigana ni kati ya changamoto kubwa iliyoko mbele ya Jumuiya ya Kimataifa. Hili ni kundi ambalo linaishi katika mazingira hatarishi pamoja na kuaminishwa kupata mambo makubwa hata pengine kinyume kabisa cha umri wao. Ni watoto wanaofundishwa kuvuta bangi katika umri mdogo, kuanza tabia chafu ya kubaka wasichana na wanawake pamoja na kuua bila huruma. RealAudioMP3

Askari yoyote mwenye umri chini ya miaka kumi na minane kadiri ya sheria za Umoja wa Mataifa anahesabiwa kuwa bado ni mtoto na haruhusiwi kushiriki katika masuala ya kivita, lakini ukweli wa mambo ni kwamba, kuna watoto zaidi ya laki tatu ambao wako mstari wa mbele. Hii inatokana na uzoefu unaoonesha kwamba, kuwatunza watoto ndani ya Jeshi ni rahisi kwani wao wanahitaji chakula kidogo tu na ni wepesi kushika na kutekeleza amri kutoka kwa wakuu wao.

Ni kundi linalofanyishwa kazi za suluba kama vile: kubeba mizigo, kupika na kuwateka wanawake na wasichana. Hii ni taarifa iliyotolewa hivi karibuni na Shirika la Wasalesiani huko Madrid, Hispania. Taarifa za Umoja wa Mataifa zinazonesha kwamba, katika kipindi cha Mwaka 2013 kuna makundi hamsini ya majeshi ya waasi na kuna mataifa manane yanayoendelea kuwafunza watoto kushika silaha kinyume cha sheria na kanuni za Umoja wa Mataifa.

Pale ambapo kuna kinzani na migogoro ya kivita, watoto na vijana ni rasilimali watu ya kwanza kabisa kutafutwa na kutumiwa, kama inavyojionesha katika nchi ambazo zina vita na migogoro ya kijamii sehemu mbali mbali za dunia. Kuna kundi kubwa la watoto na vijana linalopokonywa matumaini ya maisha bora zaidi kutoka katika familia zao kwa kulazimika kwenda mstari wa mbele ili kupigana vita!

Mambo makuu yanayowatumbukiza watoto katika vita na majanga mengine ya maisha ni pamoja na: umaskini na hali ngumu wanayokabiliana nayo, kiasi hata cha kukata tamaa na hivyo kukosa dira na mwelekeo sahihi wa maisha. Baadhi ya watoto hawa ni wale wanaotoka katika familia zilizotengana, watoto waliodhalilishwa utu na heshima yao, watoto ambao wameacha shule au ambao wakati mwingine wametekwa nyara. Kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kusimama kidete kupinga unyanyasaji wa watoto kwa kupelekwa mstari wa mbele!








All the contents on this site are copyrighted ©.