Simameni kidete kulinda na kutetea misingi ya haki, amani, demokrasia, maadili na
utu wema!
Miaka ishirini ya Demokrasia imekwisha gota, Familia ya Mungu pamoja na watu wote
wenye mapenzi mema nchini Afrika ya Kusini wanamshukuru Mwenyezi Mungu kwa zawadi
kubwa ya demokrasia nchini Afrika ya Kusini. Hiki kiwe ni kipindi muafaka kwa ajili
ya maandalizi makini ya Uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika nchini Afrika ya Kusini
tarehe 7 Mei 2014.
Baraza la
Maaskofu Katoliki Afrika ya Kusini katika barua yake ya kichungaji kuelekea kwenye
mchakato wa uchaguzi mkuu nchini Afrika ya Kusini, linawaalika waamini na wananchi
wote wenye mapenzi mema nchini Afrika ya Kusini kuhakikisha kwamba, wanasimama kidete
kulinda na kutetea misingi ya haki, amani, demokrasia, maadili na utu wema.
Ni
wakati wa kufutilia mbali kasoro zilizojitokeza wakati wa utawala wa ubaguzi wa rangi
nchini Afrika ya Kusini, sanjari na kuendeleza maboresho ya maisha ya wananchi wengi
wa Afrika ya Kusini wanaoendelea kuteseka kutoka na umaskini wa hali na kipato. Serikali
iendelee kuwekeza katika ukuaji wa uchumi, maboresho ya miundo mbinu na huduma msingi
kwa wananchi.
Baraza la Maaskofu Katoliki Afrika ya Kusini linabainisha kwamba,
miaka ishirini ya demokrasia imekwisha yoyoma, lakini bado kuna cheche za ubaguzi
wa rangi, dhuluma na nyanyaso kwa watoto wadogo, kuna mamillioni ya watu bado wanaandamwa
na umaskini mkubwa, magonjwa na ujinga; ujambawazi na matumizi ya nguvu bado ni matukio
yanayochafua amani na utulivu nchini Afrika ya Kusini.
Maaskofu wa Afrika ya
Kusini wanawachangamotisha waamini kusimama kidete kulinda na kutetea misingi ya Injili
kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa utu na heshima ya binadamu. Lengo ni kuhakikisha
kwamba, biashara haramu ya dawa za kulevya na binadamu pamoja na utumwa mamboleo vinakomeshwa
nchini Afrika ya Kusini.
Maaskofu wanawataka wanasiasa na wananchi wa Afrika
ya Kusini katika ujumla wao kuhakikisha kwamba, wanatekeleza dhamana na wajibu wao
kwa kujikita katika misingi ya ukweli, uwazi na uwajibikaji, kwa kuheshimiana na kusaidiana,
kwani kimsingi wananchi wote wa Afrika ya Kusini ni ndugu wamoja. Serikali inapaswa
kutumia rasilimali ya nchi kwa ajili ya mafao ya wengi.
Vikosi vya ulinzi
na usalama viwe mstari wa mbele kuwalinda raia na mali zao; waalimu wajielekeze zaidi
kutoa elimu makini kwa vijana wa kizazi kipya na wazazi wawe waalimu wa kwanza wa
tunu msingi za maisha ya kiroho na kiutu na kwamba, ni wajibu wa viongozi wa Kanisa
kuhakikisha kwamba, wanashiriki kikamilifu katika ustawi na maendeleo ya wananchi
wa Afrika ya Kusini: kiroho na kimwili kwa njia ya huduma makini!
Baraza la
Maaskofu wa Afrika ya Kusini linasema, mchakato wa demokrasi nchini humo unawahusu
na kuwagusa wananchi wote wa Afrika ya Kusini na wala si tu jukumu la wanasiasa wachache
ndani ya Jamii. Kila mwananchi wa Afrika ya Kusini anapaswa kuchangia kwa hali na
mali maendeleo na ustawi wa nchi yake.
Kuhusiana na uchaguzi mkuu nchini Afrika
ya Kusini, Maaskofu wanawaomba wananchi kuhakikisha kwamba, wanawapigia kura viongozi
wa kisiasa wanaosimama kidete kulinda na kutetea utakatifu wa maisha ya mwanadamu;
tunu msingi za maisha ya ndoa na familia; watu wanaowajibika, tayari kutoa kipaumbele
kwa ajili ya mafao ya wengi; watu wanaojibidisha kwa ajili ya kujenga na kudumisha
umoja, upendo, usawa na mshikamano wa kitaifa, bila kuwasahau maskini na wote wanaosukumizwa
pembezoni mwa Jamii.
Sera za vyama vya kisiasa hazina budi kujielekeza katika
mchakato wa maboresho ya huduma makini za kijamii. Ukabila, udini, rushwa na ubadhirifu
wa mali ya umma havina nafasi kwa ujenzi wa dekomrasia ya kweli nchini Afrika ya Kusini
wanasema Maaskofu.
Mwishoni, Baraza la Maaskofu Katoliki Afrika ya Kusini
linawaalika waamini na wanchi wote wa Afrika ya Kusini kumshukuru Mungu kwa zawadi
ya demokrasia katika kipindi cha miaka ishirini iliyopita. Waamini waendelee kusali
kwa ajili ya kuiombea nchi yao, ili watu waweze kuwa na matumaini, amani, umoja, upendo
na mshikamano wa dhati.
Imeandaliwa na Padre Richard A. Mjigwa, C.PP.S. Idhaa
ya Kiswahili ya Radio Vatican.