2014-02-25 09:02:32

Papa Francisko aunda Taasisi za kusimamia na kuratibu shughuli za uchumi na fedha ya Kanisa


Mama Kanisa amepewa dhamana ya kusimamia kwa uaminifu na busara mali ambayo amekabidhiwa kama sehemu ya utekelezaji wa utume wake wa Uinjilishaji, kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.Usimamizi na uratibu mzuri wa mali ya Vatican una uhusiano wa pekee na utume wa Khalifa wa Mtakatifu Petro kwa ajili ya Kanisa la Kiulimwengu sanjari na maendeleo ya mtu mzima: kiroho na kimwili.

Kwa maneno haya Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu tarehe 24 Februari 2014 ameanzisha muundo mpya wa uchumi na uratibu wa shughuli za Vatican, baada ya kufanya marekebisho makubwa kuhusiana na Waraka wa Kitume wa Mchungaji Mwema, Pastor Bonus. Baada ya kupokea ushauri wa Makardinali kwa hiyari yake mwenyewe ameamua kuunda Baraza la Kipapa la Uchumi litakalosimamia na kuratibu shughuli zote za uchumi na fedha mjini Vatican pamoja na kusimamia taasisi zote zilizoko chini ya Vatican.

Baraza la Kipapa la Uchumi litakuwa na wajumbe kumi na watano, kati yao kutakuwepo na Makardinali au Maaskofu wanane watakaoteuliwa kutoka sehemu mbali mbali za dunia, kama kielelezo cha uwakilishi wa Kanisa la Kiulimwengu, wajumbe wengine saba watakuwa ni wataalam walei watakaoteuliwa kutoka katika mataifa mbali mbali: hawa wanapaswa kuwa na sifa, ujuzi na weledi katika masuala ya fedha na uchumi.

Baraza la Kipapa la Uchumi litasimamiwa na Kardinali ambaye atakuwa na dhamana ya kuratibu shughuli zote.

Baba Mtakatifu Francisko ameunda pia Sekretarieti ya Uchumi itakayokuwa inawajibika moja kwa moja kwa Khalifa wa Mtakatifu Petro katika utekelezaji wa majukumu yake kwa kuunda sera, kanuni na taratibu za manunuzi sanjari na ugavi bora wa rasilimali watu kwa kuzingatia mahitaji ya taasisi husika. Sekretarieti ya Uchumi itasimamiwa na Kardinali, kwa kushirikiana na Sekretarieti ya Vatican na kwamba, Katibu mkuu wa Sekretarieti atakuwa na dhamana ya kumsaidia Kardinali ambaye ataratibu shughuli zote hizi.







All the contents on this site are copyrighted ©.