2014-02-25 12:15:33

Msifanye mazoea na vita!


Inasikitisha kuona umati mkubwa wa watoto wanakufa kwa njaa na utapiamlo kwenye kambi za wakimbizi, wakati ambapo watengenezaji na wafanyabiashara ya silaha wanaendelea kuponda maisha. Kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano.

Kamwe watu wasikubali vita kuwa ni sehemu ya mazoea yao na mambo yanayopamba taarifa za vyombo vya habari kwani hii ni kashfa kwa watu wa nyakati hizi: wivu na tamaa ya madaraka na utajiri wa haraka haraka ni kati ya mambo yanayochangia kuenea kwa vita sehemu mbali mbali za dunia. Watu wamekosa fadhila ya unyenyekevu na majadiliano na matokeo yake wanataka kuheshimiwa na kuabudiwa, matokeo yake ni vita na kinzani za kijamii.

Vita kwa sasa imekuwa ni kati ya mambo ya kawaida. Jumuiya ya Kimataifa kila mwaka inafanya kumbu kumbu ya vita kuu ya dunia, lakini leo hii kuna vita inayoendelea katika mataifa mbali mbali lakini hakuna mtu anayekwazika. Ndugu wanauwana kutokana na wivu, ubaguzi wa kikabila, vita na uchu wa mali na madaraka. Watu hawana budi kujenga ndani mwao ari na moyo wa amani na kuachana kabisa na falsafa ya vita inayoendelea kusababisha maafa makubwa kwa watu wasiokuwa na hatia.

Hii ni sehemu ya mahubiri ya Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu kwenye Kikanisa cha Mtakatifu Martha kilichoko mjini Vatican, siku ya Jumanne, tarehe 25 Februari 2014. Baba Mtakatifu anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kumwongokea Mwenyezi Mungu na kusali kwa ajili ya kuombea amani.

Watu watambue udhaifu wao, ili waweze kukimbilia huruma na upendo wa Mungu; wasikitishwe na maafa ya watu wasiokuwa na hatia. Watu wasifanye mazoea na vita!







All the contents on this site are copyrighted ©.