2014-02-25 09:26:55

Kardinali George Pell ateuliwa kuwa ni Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa linaloratibu masuala ya uchumi na fedha


Baba Mtakatifu Francisko amemteua Kardinali George Pell, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Sydney, Australia kuwa Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa linaloratibu Uchumi na Fedha ya Vatican baada ya kupata ushauri kutoka kwa Makardinali katika mkutano wao uliohitimishwa hivi karibuni mjini Vatican.

Kardinali Pell alizaliwa kunako tarehe 8 Juni 1941. Baada ya masomo na majiundo yake ya Kikasisi, alipadrishwa kunako tarehe 16 Desemba 1966. Tarehe 21 Mei 1987 akawekwa wakfu kuwa Askofu msaidizi wa Jimbo kuu la Melbourne, Australia. Tarehe 16 Julai 1996 Papa Yohane Paulo wa Pili akamteuwa kuwa Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Melbourne. Tarehe 26 Machi 2001 akateuliwa kuwa ni Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Sydney. Tarehe 28 Septemba 2003 akasimikwa kuwa ni Kardinali.

Kardinali Pell ni kiongozi mwenye uzoefu mkubwa katika masuala ya uchumi na fedha. Amekuwa ni kati ya Makardinali washauri wa Papa Francisko katika mchakato wa marekebisho ya kina mjini Vatican. Amekuwa ni kiongozi aliyejipambanua katika mikakati ya maendeleo ya mtu mzima: kiroho na kimwili; mshauri katika masuala ya maadili ya biashara, haki jamii pamoja na maisha ya hadhara.







All the contents on this site are copyrighted ©.