2014-02-24 11:40:23

Tumieni busara, ukweli na uzuri unaofumbatwa katika Injili ili kugusa akili na mioyo ya watu wanaotafuta maana ya maisha!


Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa washiriki wa mkutano wa SIGNIS unaofunguliwa rasmi tarehe 25 Februari 2014 mjini Roma, ulioandikwa kwa niaba yake na Kardinali Pietro Parolin, Katibu mkuu wa Vatican anasema, vyombo vya mawasiliano ya kijamii vinachangia kujenga uzoefu, matumaini na mashaka miongoni mwa vijana wa kizazi kipya.

Huu ni ulimwengu wa utandawazi unaofumbata tamaduni, lugha na vielelezo vipya vinavyoonesha mwingiliano wa kijamii. Waamini wa Kanisa Katoliki wanaotekeleza dhamana na wajibu wao katika vyombo vya Upashanaji habari wanaendelea kuchangamotishwa kutumia: busara, ukweli na uzuri unaofumbatwa katika Injili ili kugusa akili na mioyo ya watu ambao wana kiu ya maana ya maisha na wanataka kuwa na mwongozo kamili katika maisha yao ndani ya Jamii.

Baba Mtakatifu anaonesha matumaini yake kwamba, mkutano huu utawawezesha wajumbe kupata mwelekeo mpya pamoja na ujasiri wa kusonga mbele kwa imani na matumaini ili kukabiliana na changamoto zinazoendelea kujitokeza katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari.







All the contents on this site are copyrighted ©.