2014-02-21 11:20:52

Salini kwa ajili ya Khalifa wa Mtakatifu Petro wakati wa Siku kuu ya Ukulu wa Mtakatifu Petro


Baba Mtakatifu Francisko, Jumamosi tarehe 22 Februari 2014 katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Ukulu wa Mtakatifu Petro, anatarajiwa kuongoza Ibada ya Neno la Mungu kwa kuwasimika Makardinali wapya 19 aliowateuwa hivi karibuni kutoka sehemu mbali mbali za dunia.

Ni tukio ambalo litakuwa na sehemu kuu tatu: sehemu ya kwanza: Makardinali wapya watapewa kofia nyekundu za Ukardinali; pili watapewa pete ya Ukardinali na tatu, watakabidhiwa Makanisa ya huduma mjini Roma kwani kwa kutangazwa kuwa Makardinali wanakuwa ni wasaidizi na washauri wakuu wa Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Ibada itakayotumika Jumamosi wakati wa kuwasimika Makardinali ni ile ambayo imefanyiwa Marekebisho makubwa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita. Ikumbukwe kwamba, Ukardinali si Sakramenti bali ni heshima ambayo Kanisa linawatunukiwa baadhi ya watoto wake kwa ajili ya kusaidia mchakato wa kuliongoza Kanisa la Kristo. Kardinali mteule Pietro Parolin ndiye atakayetoa neno la shukrani kwa Baba Mtakatifu Francisko kwa niaba ya Makardinali wenzake wote, siku ya Jumamosi.

Baba Mtakatifu Francisko, Jumapili ijayo tarehe 23 Februari 2014 ataadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Petro akiwa amezungukwa na Makardinali wapya.

Baba Mtakatifu Francisko anawaalika waamini pamoja na watu wote wenye mapenzi mema, kusali kwa ajili ya kumwombea ili aweze kutekeleza vyema dhamana na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro; tayari kushuhudia kwa njia ya imani tendaji ujenzi wa Kanisa la Kristo.







All the contents on this site are copyrighted ©.