2014-02-20 09:25:14

Mambo msingi yanayogusa utu na heshima ya binadamu!


Zawadi ya uhai, tunu msingi za maisha ya ndoa na familia; uhuru, dhamana na wajibu wa wazazi na walezi katika majiundo makini ya watoto wao pamoja na umuhimu wa kusimama kidete kulinda na kudumisha mafao ya wengi ni kati ya mambo makuu yaliyojitokeza kwenye ujumbe wa Baraza la Maaskofu Katoliki Italia katika Maadhimisho ya Siku ya Uhai Kitaifa, iliyoadhimishwa, hivi karibuni. Haya ni mambo msingi yanayogusa utu na heshima ya mwanadamu bila kusahau mchango wa Kanisa katika sekta ya elimu. RealAudioMP3
Waamini na watu wenye mapenzi mema nchini Italia wanaendelea kuhamasishwa kusimama kidete kulinda na kutetea Injili ya Uhai dhidi ya utamaduni wa kifo; uhuru usiokuwa na mipaka wala kuzingatia maadili na utu wema. Sheria zinazotaka kufuta tofauti msingi za kijinsia kwa ajili ya kulinda uhuru wa baadhi ya wananchi ni kuhatarisha maana, dhamana na mchango wa maisha ya ndoa na familia.
Matumizi ya maneno “Baba” na “Mama” bado ni muhimu sana katika kudumisha tunu msingi za maisha ya ndoa na familia. Kumbe, kuna haja kwa wanasiasa kuwa makini katika mikakati ya majiundo ya vijana wa kizazi kipya, kwa kukuza na kuunda dhamiri nyofu, ili kutoa nafasi kwa vijana kutambua mema ya kufuata na mabaya ambayo wanapaswa kuepukana nayo. Ni jambo la kusikitisha kuona kwamba, wanasiasa wanakimbilia kutunga sheria zinazohatarisha tunu msingi za maisha ya ndoa na familia wanasema Maaskofu Katoliki Italia.
Jamii inapaswa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa utu na heshima ya binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Kila mwanadamu anapaswa kulindwa na kuheshimiwa, lakini zaidi kwa wale wasiokuwa na sauti, kwa kuondokana na sera za ubaguzi, nyanyaso na madhulumu kwa wanawake. Maaskofu wa Italia wanasema, Ndoa kati ya Bwana na Bibi ni matunda ya upendo wa dhati kati ya mume na mke, wanaotambua kwamba, wanashirikishwa kwa namna ya pekee katika kazi ya Uumbaji na malezi ya watoto wao.
Kimsingi wazazi ni walinzi wa zawadi ya maisha, tunu msingi za maisha ya ndoa na familia pamoja na elimu makini kwa watoto wao. Kamwe wanasiasa wasitake kuwavuruga wananchi kwa kuanzisha dhana na mambo ambayo hayana mafao wala mashiko kwa mtu binafsi na Jamii kwa ujumla.
Baraza la Maaskofu Katoliki Italia linaangalisha kwamba, haiwezekani kuanzisha siasa za usawa wa kijinsia inayosigana na ukweli msingi wa tofauti zilizopo kati ya mwanaume na mwanamke, kiasi cha kulinda mwelekeo huu potofu kwa njia ya sheria. Maaskofu wanapenda bado kusikia watu wakitumia maneno “mke wangu”, “Baba”, “Mama” au “Mume wangu”; dhana inayofumbatwa katika maisha ya ndoa na familia kati ya mume na mke. Huu ndio utashi wa Mungu katika maisha ya binadamu katika mchakato wa kumshirikisha katika kazi ya Uumbaji.
Baraza la Maaskofu Katoliki Italia linaendelea kuwatia shime waamini na watu wenye mapenzi mema wanaotekeleza wajibu wao katika mazingira na changamoto kubwa kama hizi, kutoka tamaa bali kusonga mbele kwa ari na moyo mkuu, huku wakishuhudia tunu msingi za maisha ya ndoa na familia; tofauti za kijinsia kati ya mume na mke; uhuru wa kidini na umuhimu wa wazazi na walezi katika kushiriki kikamilifu katika mchakato wa elimu na majiundo makini ya watoto wao: kiroho na kimwili.
Kanisa daima linapenda kulinda na kutetea mafao ya wengi ndani ya Jamii. Zawadi ya uhai katika hatua zake msingi ni mambo yanayopewa kipaumbele cha kwanza na Kanisa, kwani linatambua kwamba, uhai ni zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Maaskofu wanapenda kuonesha mshikamano wao wa dhati na wananchi wote wa Italia wanakabiliana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa. Wanawasihi kwamba, licha ya magumu na changamoto mbali mbali za maisha, waendelee kusimama kidete kulinda na kutetea Injili ya Uhai.








All the contents on this site are copyrighted ©.