Maaskofu wa Kipentekoste walalama kuhusu ushiriki wao katika Bunge Maalum la Katiba
Tanzania
Taarifa ya ufafanuzi kuhusu Baraza la Maaskofu wa Kipentekoste Tanzania (Pentecostal
Council of Tanzania) kutokuwa na uwalikilishi katika bunge maalum la katiba.
1.
Uteuzi wa Wajumbe wa Bunge la Katiba unafanywa kwa mujibu wa Sheria ya Mabadiliko
ya Katiba, Sura, 83 (The Constitutional Review Act, Cap 83). Sheria hii inaweka mamlaka
ya uteuzi, masharti, taratibu, vigezo na mambo mengine yote yanayopaswa kuzingatiwa
katika uteuzi wa Wajumbe wa Bunge la Katiba. Kwa mujibu wa Kifungu cha 22 (2A) na
(2B) vigezo hivi vinajumuisha umri, jinsia, uzoefu, sifa na mahali anapotoka mjumbe
husika.
2. Sheria hii imeainisha aina tatu za Wajumbe wa Bunge la
Katiba kama ifuatavyo: (i) Wabunge wote wa Bunge la Jamhuri ya Muungano; (ii)
Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar; na (iii) Wajumbe 201 kwa
mujibu wa Kifungu Na. 22(1c) cha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ambayo inaonyesha
makundi mbalimbali 10 yanayohusika.
3. Kwa mujibu wa Sheria ya Mabadiliko
ya Katiba, wajumbe 201 wanatakiwa kuteuliwa kutoka katika makundi yafuatayo: (i)
Taasisi zisizokuwa za Kiserikali (20) (ii) Taasisi za Kidini (20) (iii)
Vyama vyote vya Siasa vyenye Usajili wa Kudumu (42); (iv) Taasisi za
Elimu (20); (v) Watu wenye Ulemavu (20); (vi) Vyama
vya Wafanyakazi (19); (vii) Vyama vinavyowakilisha Wafugaji (10); (viii)
Vyama vinavyowakilisha wavuvi (10); (ix) Vyama vya Wakulima (20); na (x)
Vikundi vya Watu wenye Malengo yanayofanana (20).
4. Mchakato wa
uteuzi ulianza kwa kutoa Tangazo la Mwaliko katika Gazeti la Serikali, Tangazo la
Serikali Na. 443 la tarehe 13 Desemba, 2013. Tangazo hilo lilitolewa kwa lugha ya
Kiswahili na Kiingereza ili kuyaalika makundi yaliyotajwa kisheria kuwasilisha mapendekezo
ya majina kwa ajili ya uteuzi katika Bunge Maalum la Katiba. Aidha, Tangazo hilo lilitangazwa
pia katika magazeti mbalimbali yanayosomwa hapa nchini. Pamoja na mambo mengine, Tangazo
hilo lilitamka ukomo wa muda wa taasisi na makundi kuwasilisha mapendekezo ya majina
ya wajumbe kuwa ni tarehe 02 Januari 2014.
5. Mapendekezo hayo yalitakiwa
kuwasilishwa kwa Katibu Mkuu Kiongozi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
au kwa Katibu Mkuu Kiongozi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar. Mapendekezo hayo yalitakiwa
kuwasilishwa kwa njia ya barua ya posta au barua inayoletwa kwa mkono. Sheria haikutoa
njia nyingine ya kuwasilisha mapendekezo. Ninafahamu, wengine wangeweza kutumia barua
pepe au hata ujumbe mfupi wa maneno. Sheria haisemi hivyo!
6. Kufuatia
mwaliko huo, taasisi 554 kutoka Tanzania Bara na 178 kutoka Zanzibar ziliwasilisha
mapendekezo yao. Mapendekezo hayo yalijumuisha majina 2,762 kwa upande wa Tanzania
Bara na kwa upande wa Zanzibar mapendekezo hayo yalihusisha watu 874. Hivyo basi,
taasisi na makundi mbalimbali yalipendekeza jumla ya majina 3,636. Aidha, watu 118
walijipendekeza wenyewe kinyume na matakwa ya kisheria na kufanya idadi ya majina
yaliyopendekezwa kuwa 3,754.
7. Sheria ya Mabadiliko ya Katiba imeweka
masharti katika uteuzi wa wajumbe 201 wa Bunge Maalum la Katiba. Masharti hayo, ni
pamoja na wajumbe wasiopungua theluthi moja wanatakiwa kutoka Zanzibar na theluthi
mbili kutoka Tanzania Bara. Kwa sababu hiyo, katika wajumbe 201, wajumbe 67 wanatakiwa
kutoka Zanzibar na wajumbe 134 wanatakiwa kutoka Tanzania Bara. Aidha, uteuzi huo
unatakiwa kuzingatia idadi ya wajumbe kutoka katika kila kundi kama ilivyoainishwa
kisheria. Vilevile, mgawanyo wa wajumbe wanawake na wanaume unatakiwa uwe nusu kwa
nusu. Pamoja na hayo, wajumbe hao wawakilishe sura ya wananchi wa Tanzania kwa ufuasi
wa vyama vya siasa, dini, umri, na maeneo wanayotoka.
8. Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akishirikiana na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa
Baraza la Mapinduzi Zanzibar walikamilisha uteuzi wa wajumbe 201 na majina ya walioteuliwa
yalitangazwa tarehe 7 Februari 2014. Majina hayo yalitangazwa kupitia taarifa kwa
vyombo vya habari na pia Gazeti la Serikali kwa Tangazo la Serikali Na. 29 la tarehe
7 Februari 2014.
BARAZA LA MAASKOFU WA KIPENTEKOSTE TANZANIA
9.
Tarehe 11 Februari 2014, Baraza la Maaskofu wa Kipentekoste Tanzania lilitoa taarifa
kwa vyombo vya habari kuhusu uteuzi wa Wabunge wa Bunge Maalum la Katiba. Baraza liliomba
vyombo vya habari lifikishe masikitiko ya Baraza kwa viongozi na waamini wa Kipentekoste
wote na jamii ya wapenda haki hapa nchini, kutokana na kitendo cha Serikali wanayoiheshimu,
wanayoipenda na kuiombea, kwa kulibagua na kulitenga Baraza lisihusike na Bunge Maalum
la Katiba.
10. Katika Taarifa yake kwa vyombo vya habari, Baraza la Maaskofu
wa Kipentekoste Tanzania limeeleza kuwa kwa …”utaratibu tuliojiwekea katika utawala
wa Baraza letu, hakuna Kanisa moja, mchungaji binafsi, mwamini, anaweza kujitwalia
heshima, kuchukuliwa au kupewa haki na chombo chochote cha Serikali katika nchi yetu
kwa nia ya kuwakilisha wapentekoste, bila kupata idhini toka kikao halali cha Kamati
Kuu ya Utendaji ya PCT-Taifa”.
11. Kwa kuzingatia utaratibu huu “Kamati
Kuu ya Utendaji ya PCT-Taifa katika kikao chake cha tarehe 5/12/2013 ilipendekeza
kwa Mheshimiwa Rais majina ya wajumbe wake iliowaona kuwa wanafaa kuchaguliwa katika
Bunge Maalum la Katiba, lakini cha kusikitisha kati ya hao hakuna jina la mjumbe hata
mmoja ambaye alichaguliwa na Mheshimiwa Rais katika Bunge Maalum la Katiba”.
12.
Taarifa hiyo imeeleza pia, “… Serikali imeona hatufai na hatuna sifa za kuweza kuchaguliwa
katika Bunge Maalum la Katiba, na badala yake ikaamua kuteua majina ya wajumbe toka
katika taasisi nyingine za kidini zenye hadhi kama yetu za Waislamu, Wakatoliki, Waprotestanti
na Wajumbe wengine binafsi kwa Tanzania Bara na Visiwani na kuwaacha Wapentekoste…”
UFAFANUZI
WA SERIKALI 13. Kwanza kabisa, napenda kuwahakikishia watanzania na hasa wale
waliolengwa na taarifa ya Baraza, kwamba Serikali haikuupuzia kundi lolote lililoanishwa
kwa mujibu wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba kuwasilisha mapendekezo ya wajumbe wa
Bunge Maalum la Katiba. Serikali inaliheshimu Baraza na tunalishukuru sana katika
juhudi inazozifanya kwa pamoja na Serikali katika kuwaendeleza wananchi wa Tanzania.
14.
Kutokana na umuhimu wa makundi mbalimbali, jumla ya makundi 850 yaliwasilisha mapendekezo
ya majina 3,636. Katika makundi haya 850, kulikuwa na mapendekezo kutoka taasisi au
makundi ya kidini 72 ambayo yalipendekeza jumla ya majina 429. Kwa upande wa Tanzania
Bara, taasisi za kidini 55 ziliwasilisha mapendekezo yenye jumla ya majina 344. Aidha,
Serikali ilipokea mapendekezo 118 kutoka kwa waliojipendekeza wenyewe! Hivyo, siyo
kweli kuwa Serikali ilipuuza mapendekezo kutoka kundi fulani ikiwa ni pamoja na Baraza
la Maaskofu wa Kipentekoste Tanzania. Serikali hii ni kwa ajili ya watu na makundi
yote. Aidha, Katiba yetu haibagui watu au makundi ya watu kwa lengo la kuwanyima au
kuwakosesha haki.
15. Kufuatia taarifa ya Baraza la Maaskofu wa Kipentekoste
Tanzania kwa vyombo vya habari kuwa mapendekezo yao yamepuuzwa, kwa kuanzia Serikali
imefuatilia kama kweli Baraza hilo liliwasilisha mapendekezo. Kwa kuwa mapendekezo
yote yaliyowasilishwa yaliwekwa katika kanzi data ya msingi (primary data base) kwa
ajili ya uchambuzi, utafutaji kwa kutumia kompyuta (computer search or find) ulifanywa
ili kubaini kama kulikuwa na mapendekezo kutoka Baraza kati ya mapendekezo 850 yaliyowasilishwa.
16.
Kwa kuwa hakukuwa na taarifa za majina ya waliopendekezwa, jina la taasisi na majina
ya maaskofu watano (5) walioshiriki katika utoaji taarifa kwa vyombo vya habari yalitumika
katika kubaini kama wao pia walikuwa miongoni mwa waliopendekezwa. Utafutaji wa huu
haukubaini kuwa Baraza ilikuwa moja ya taasisi zilizowasilisha maombi. Aidha, hapakuwa
na jina hata moja la viongozi wa Baraza walioitisha vyombo vya habari kutoa taarifa.
17. Pamoja na kwamba haikutarajiwa kuwa viongozi wa taasisi hii kujipendekeza
wenyewe, na hivyo kuwa miongoni mwa watu 118 waliojipendekeza wenyewe, juhudi za Serikali
zilijielekeza kutafuta endapo kulikuwa na mapendekezo kundi hili. Hata hivyo, utafutaji
haukubaini majina ya viongozi hawa kuwepo katika orodha hiyo.
18. Kulikuwa
na uwezekano pia, Baraza liliwasilisha mapendekezo ambayo yalifika kwa Katibu Mkuu
Kiongozi nje ya muda uliopangwa kisheria wa tarehe 2 Januari 2014. Uchambuzi wa mapendekezo
52 ambayo yaliwasilishwa nje ya muda haukubaini kuwepo kwa mapendekezo kutoka Baraza
la Maaskofu wa Kipentekoste Tanzania.
19. Hivyo, juhudi za Serikali katika
kufuatilia uwepo wa mapendekezo kutoka Baraza la Maaskofu wa Kipentekoste Tanzania
hazikuweza kuthibitisha kuwa Baraza lilituma mapendekezo yake kama ilivyokuwa imeagizwa
na Sheria ya mabadiliko ya Katiba!
UWAKILISHI WA MADHEHEBU YANAYOUNDA BARAZA
LA MAASKOFU WA KIPENTEKOSTE TANZANIA
20. Kwa kufahamu umuhimu wa makundi
mbalimbali ya kidini ikiwa ni pamoja na Baraza la Maaskofu wa Kipentekoste Tanzania
unaoundwa na Maaskofu Wakuu wa madhehebu ya kipentekoste yapatayo 75, uteuzi wa wajumbe
wa Bunge Maalum la Katiba ulihakikisha kuwa makundi ya kidini yanawakilishwa ipasavyo.
21.
Mgawanyo wa idadi ya wajumbe 20 kutokana na makundi ya kidini baina ya Tanzania Bara
na Zanzibar kwa kuzingatia uwiano wa moja ya tatu ya wajumbe kutoka Zanzibar ulimaanisha
kuwa katika kundi hili, wajumbe 7 wangekuwa wanatoka Zanzibar na wajumbe 13 wangekuwa
wanatoka Tanzania Bara. Uteuzi wa wajumbe katika kundi hili umezingatia kigezo hiki.
22.
Kufuatia uteuzi uliofanywa tarehe 7 Februari 2014, uchambuzi wa majina ya wajumbe
wa Bunge Maalum la Katiba umebaini kuwa kati ya wajumbe 13 kutoka taasisi za kidini
wa Tanzania Bara walioteuliwa, mjumbe mmoja (1) aitwaye Bibi Respa Miguma Adam ameteuliwa
kutoka Evangelistic Assemblies of God Tanzania (EAGT), Patmos Vision, Kigamboni Church.
Evangelistic Assemblies of God Tanzania ni moja ya madhehebu ambayo maaskofu wake
wakuu wanaunda Baraza la Maaskofu wa Kipentekoste Tanzania.
23. Hivyo,
tamko la Baraza la Maaskofu wa Kipentekoste kuwa wanabaguliwa halina ukweli kwa kuwa
uchunguzi tulioufanya haujathibitisha kuwa Baraza lilileta mapendekezo. Ni vyema Baraza
likafanyia kazi kwa nini kama kulikuwa na mapendekezo, hayakufikishwa kwa Katibu Mkuu
Kiongozi (Dar es Salaam) au Katibu Mkuu Kiongozi (Zanzibar). Ninaamini kabisa kama
mapendekezo hayo yangekuwa yamewasilishwa, Mhe. Rais angechagua mwakilishi kutokana
na mapendekezo hayo.
HITIMISHO 24. Uteuzi wa Wajumbe
wa Bunge Maalum la Katiba uliofanywa na Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
kwa kushirikiana na Mhe. Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar
tarehe 7 Februari 2014, kwa namna yoyote ile haukuwa na nia ya kulibagua Baraza la
Maaskofu wa Kipentekoste Tanzania.
25. Kuna kila sababu ya kuamini kuwa
mapendekezo ya Wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba kutoka Baraza la Maaskofu wa Kipentekoste
Tanzania hayakuwasilishwa kwa Katibu Mkuu Kiongozi kama sheria ilivyohitaji. 26.
Pamoja na kuwa Baraza la Maaskofu wa Kipentekoste Tanzania hawakuweza kuwasilisha
mapendekezo yao kama ilivyotakiwa, tunaamini kuwa Baraza, kama ilivyo kwa wananchi
wote, litawakilishwa vyema na wajumbe walioteuliwa ambao wanajumuisha mjumbe aliyeteuliwa
kutoka moja ya madhehebu yanayounda Baraza la Maaskofu wa Kipentekoste Tanzania.