2014-02-20 11:14:53

Jitokezeni kushiriki kwenye uchaguzi mkuu hapo tarehe 7 Mei 2014


Baraza la Maaskofu Katoliki Afrika ya Kusini linawahamasisha waamini na wananchi wote wa Afrika ya Kusini katika ujumla wao kuhakikisha kwamba, wanashiriki kikamilifu katika kupiga kura hapo tarehe 7 Mei 2014. Hii ni haki ambayo wananchi wa Afrika ya Kusini wameipata baada ya watu wengi kumwaga damu yao ambayo imekuwa ni mbegu ya demokrasia katika kipindi cha miaka ishirini tangu utawala wa ubaguzi wa rangi ulipoondolewa nchini Afrika ya Kusini.

Huu utakuwa ni uchaguzi mkuu wa tano kufanyika nchini Afrika ya Kusini baada ya kuanguka kwa utawala wa ubaguzi wa rangi. Wananchi wa Afrika ya Kusini wanaweza kuamua kufanya mageuzi kwa njia ya kura zao. Afrika ya Kusini bado inaendelea kukabiliana na cheche za ubaguzi, umaskini wa hali na kipato, ukosefu wa fursa za ajira, miundo mbinu mibovu, huduma hafifu za kijamii, uhalifu pamoja na kudorora kwa elimu inayotolewa nchini Afrika ya Kusini.

Licha ya mapungufu haya yaliyojitokeza katika kipindi cha miaka ishirini iliyopita, lakini Baraza la Maaskofu Katoliki Afrika ya Kusini linasema kwamba, kumekuwepo pia na mafanikio ya kuridhisha katika maboresho ya makazi ya watu, huduma bora ya maji safi na salama kwa idadi kubwa ya wananchi wa Afrika ya Kusini; ujenzi wa miundo mbinu ya barabara na maboresho katika huduma za afya.

Haya ni matunda ya mchakato wa kidemokrasia yaliyofikiwa na wananchi wa Afrika ya Kusini. Ndiyo maana Maaskofu wanawahimiza wananchi wa Afrika ya Kusini kujitokeza kwa wingi kushiriki katika mchakato wa uchaguzi mkuu nchini Afrika ya Kusini.







All the contents on this site are copyrighted ©.