2014-02-19 08:47:07

Majina ya wenyeheri watarajiwa!


Baba Mtakatifu Francisko hivi karibuni ameridhia kuchapwa kwa nyaraka mbali mbali zinazowahusu watumishi wa Mungu na wenyeheri katika mchakato wa kutangazwa kuwa watakatifu kama zilivyowasilishwa kwake na Kardinali Angelo Amato, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la kuwatangaza waamini kuwa wenyeheri na watakatifu. Kati yao kuna: RealAudioMP3

Mtumishi wa Mungu Padre Piet Asua Mendia, kutoka Hispania, aliyezaliwa tarehe 30 Agosti 1890 na kuuwawa kutokana na chuki za kidini tarehe 29 Agosti 1936.

Mtumishi wa Mungu Padre Giuseppe Girelli kutoka Jimbo la Verona, Italia, aliyezaliwa tarehe 10 Januari 1886 na kufariki dunia Mei Mosi 1978 kutokana na ushupavu wake wa kiimani.

Kanisa limetambua karama ya ushupavu wa kiimani ulioneshwa na Mtumishi wa Mungu Padre Zaccaria di Santa Teresa wa Shirika la Wakrameli, aliyezaliwa kunako tarehe 5 Novemba 1887 na kufariki dunia tarehe 23 Mei 1957, akiwa nchini India.

Mama Kanisa ametambua ushupavu wa kiimani ulioshuhudiwa na Mtumishi wa Mungu Marcella Mallet, Mwanzilishi wa Shirika la Masista wa Upendo, Quebec, aliyezaliwa tarehe 26 Machi 1805 na kufariki dunia hapo tarehe 9 Aprili 1871.

Wengine katika orodha hii ni pamoja na Mtumishi wa Mungu Maria Benadetta Aria, Mwanzilishi wa Shirika la Masista wahudumu wa Yesu katika Sakramenti, aliyezaliwa tarehe 3 Aprili 1822 huko Buenos Aires, Argentina na kufariki dunia tarehe 25 Septemba 1894 kutoka na ushupavu wake wa kiimani.

Kanisa linatambua ushupavu wa kiimani uliojidhihirisha katika maisha ya Mtumishi wa Mungu Margharita wa Moyo Mtakatifu wa Yesu, Mwanzilishi wa Shirika la Masista Wafranciskani wa Moyo Mtakatifu wa Yesu, aliyezaliwa kunako tarehe 28 Novemba 1862 huko Malta na kufariki dunia tarehe 22 Januari 1952.

Mama Kanisa anatambua fadhila za ushupavu wa kiimani zilizooneshwa kwa namna ya pekee katika maisha ya Mtumishi wa Mungu Serafina wa Shirika la Masista Waabuduo Damu Takatifu ya Yesu, aliyezaliwa tarehe 31 Januari 1913 na kufariki dunia hapo tarehe 21 Oktoba 1988 huko Manaus, Brazil.

Mwishoni, Kanisa limetambua pia fadhila za kiimani zilizojitokeza katika maisha ya Mtumishi wa Mungu Elizabeth Sanna, mjane na mwamini mlei, aliyejifunga kwa nadhiri katika Utawa wa watu wa Mtakatifu Francisko katika huduma ya upendo na mshikamano ulioanzishwa na Mtakatifu Vinzent wa Paolo. Yeye alizaliwa tarehe 23 Aprili 1788 Sassari, Italia na kufariki dunia tarehe 17 Februari 1857 mjini Roma.








All the contents on this site are copyrighted ©.