2014-02-17 09:28:06

Vizuizi vya ndoa!


Mpendwa Msikilizaji wa Radio Vatican endelea kutega sikio tuhekimishane kuhusu yale yahusuyo maisha ya ndoa na familia. Kwa vipindi kama hivi, Kanisa linaendelea kutekeleza wajibu wake wa kuwafundisha, kuwaombea na kuwasaidia wote walioitikia wito wa ndoa ili waweze kutekeleza vema malengo ya wito huo. RealAudioMP3

Katika kipindi hiki, tushirikishane juu ya vizuizi vya ndoa kadiri ya sheria ya Kanisa. Mpendwa msikilizaji, ili somo letu lisiwe zito masikioni, tutaichambua mada hii kwa mtazamo wa kichungaji zaidi. Tunaiweka kwa ufupi sana na kwa mifano myepesi. Undani wake mwaweza kupata katika semina za ndoa. Kwa yale ambayo hayataweza kufafanulika vizuri hadharani hapa, tunawaalikeni nyote waendeeni Maparoko na Mapadre wetu, waulizeni nao watawahekimisha.

Mpendwa msikilizaji, kwa wale wenye kufuatilia mada hii katika Ngombo la Sheria za Kanisa, tafakari hii ina uhalali kwa nguvu sheria ya Kanisa, Kanuni namba 1083 – 1094. Hapo tunakuta vizuizi KUMI NA VIWILI. Kuna vizuizi ambavyo ni vya hadhara na vingine sio vya hadhara. Vipo vya kijamii na vingine ni vya kiroho. Kwaye anayetaka kuingia katika wito huo wa ndoa, kisha jua kwamba ana kizuizi, basi kitatuliwe kwa taratibu zinazokubalika.

Tunaposikia tangazo “UNGA NA MAJI WANATAKA KUFUNGA NDOA, TANGAZO LA KWANZA. Wanaojua kizuizi chochote wapashe habari katika ofisi ya Paroko, haya yafuatayo ndiyo ya kupeleka. Usipeleke habari isiyohusika, eti aah binti yule anakiburi huwa hanisalimii. Au aah yule bwana anajiona sana, mimi naona hata ndoa hiyo asifunge!! Wee, hivyo sio kizuizi kisheria. VIZUIZI VYENYEWE NI HIVI HAPA:-

Kizuizi cha kwanza ni UMRI. Sheria Kan, namb. 1083 inaelekeza kwamba, mwanaume anaweza kuoa akiwa na umri wa miaka 16, na binti anaweza kuolewa akiwa na umri wa miaka 14. Kanisa linaona umri huo kwa tamaduni nyingi, mtu anaweza kuchukua majukumu ya ndoa na kuhimili mikikimikiki ya ndoa na familia. Endapo wanandoa wana umri mdogo zaidi, kizuizi kipelekwe kwa Paroko. Hapa Kanisa limetamka tu umri wa chini. Kuhusu umri wa juu halijasema kitu na hicho sio kizuizi (Ila hali halisi itazamwe). Mtu asiseme, aah mbona mchumba mwenyewe amemzidi umri, au mbona wamepishana sana umri hawezi kumuoa. Hapana, wasiwe chini ya 16 na 14. Huko kwingine sio kizuizi.

Kizuizi cha pili ni UHANITHI. Sheria Kan, namb. 1084 inazingatia lengo la ndoa ‘kuzaa watoto’. Endapo mmoja hana uwezo wa tendo la ndoa (aweza kuwa mke au mume), huyo anazuiwa kwa sheria ya asili. Hiki ni kizuizi cha ndani, hakionekani usoni. Ni juu ya mtu binafsi kujijua.

Tutofautishe hapa kati ya kukosa uwezo wa kushiriki tendo la ndoa na kukosa uwezo wa kuzaa (utasa na ugumba). Utasa na ugumba, havizuii wala kutengua ndoa. Siku zetu hizi mang’amuzi ya kichungaji yanashuhudia kukithiri kwa tatizo la uhanithi kwa vijana wengi wa kike na wa kiume. Siku nyingine tutachambua sababu ya mkasa huu. Ukitambua kama fulani ana shida hii, basi hicho ni kizuizi, asiingie kwenye ndoa atatesa mwenzake. Lakini nyakati zetu sayansi ya tiba imekuwa sana ni vema watu kushughulikia afya zao mapema kama kuna matatizo.

Kizuizi cha tatu ni NDOA-AWALI. Sheria Kan, namb. 1085 inakataza mtu kuoa au kuolewa wakati alikwisha kufunga ndoa na ndoa ya kwanza bado ipo hai. Sasa, huweza kutokea mazingira kwamba wanandoa wametengana kwa taratibu za talaka za kiserikali. Kanisa bado linatambua na kuheshimu ile sakramenti; hivyo haliruhusu ndoa nyingine!

Changamoto ya nyakati zetu hizi, ambapo wadanganyifu ni wengi, mtu anafunga ndoa kona mmoja ya nchi, anamtoroka mwezi wake, anakwenda kona nyingine ya dunia anaoa au kuolewa huko wakati alikotoka ameacha mke au mume na watoto. Hilo agano la pili ni batili. Ukisikia ndoa inatangazwa ya mtu ambaye unajua aliwahi kuoa au kuolewa na mwenziwe yupo, kimbia kaseme, ni kizuizi hicho.

Kizuizi cha nne ni UTOFAUTI WA IMANI. Sheria Kan, namb. 1086, inaelekeza kwamba, iwapo mmoja ni Mwamini Mbatizwa Mkatoliki na mwingine sio, utofauti huo ni vema utatuliwe kwanza kadiri ya taratibu zetu. (Utofauti unaoelezwa hapa ni ule kati ya Mkatoliki na Mkristo asiye mkatoliki, au Mkatoliki na mwamimi wa dini nyinginezo). Taratibu msingi zifuatwe ili kweli iwe Sakramenti. Baba Paroko anajua cha kufanya.

Hadi hapa ndugu mzikilizaji wa Radio Vatican, tunaahirisha makala yetu kwa leo, Juma lijalo tutaendelea kuhekimishana kuhusu vizuizi vya ndoa ya Kikristo kwa kuangalia kuhusu maisha ya Daraja Takatifu, Utawa pamoja mtu kutoroshwa. Hadi wakati mwingine tena ni mimi Padre Pambo Martin Mkorwe, OSB.








All the contents on this site are copyrighted ©.